JKCI yaiweka Tanzania kileleni Afrika Mashariki na Kati kwa upasuaji wa kisasa wa kubadilisha valvu za moyo bila kufungua kifua (TAVI)


Wataalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao kutoka nchini India wakifanya upasuaji wa kisasa wa kubadilisha valvu ya moyo kwa njia ya tundu dogo bila kufungua kifua (Transcatheter Aortic Valve Implantation - TAVI) katika kambi maalumu ya siku moja ambapo wagonjwa wawili walifanyiwa upasuaji.
Wataalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao kutoka nchini India wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumfanyia mgonjwa upasuaji wa kisasa wa kubadilisha valvu ya moyo kwa njia ya tundu dogo bila kufungua kifua (Transcatheter Aortic Valve Implantation - TAVI) katika kambi maalumu ya siku moja ambapo wagonjwa wawili walifanyiwa upasuaji.
Wataalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao kutoka nchini India wakiangalia upasuaji wa kisasa wa kubadilisha valvu ya moyo kwa njia ya tundu dogo ulivyofanyika bila ya kufungua kifua (Transcatheter Aortic Valve Implantation - TAVI) katika kambi maalumu ya siku moja ambapo wagonjwa wawili walifanyiwa upasuaji.
**************************************************************************************************************************************************************************************************
Dkt. Waane alisema upasuaji huo uliofanyika
jana unajulikana kitaalamu kama Transcatheter
Aortic Valve Implantation (TAVI) hufanyika katika Taasisi chache sana
Afrika Mashariki na Kati, huku Tanzania ikiwa nchi pekee inayotoa huduma hiyo
kwa sasa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
“Upasuaji huu unafanyika kwa wagonjwa
ambao hawawezi kufanyiwa upasuaji wa kufungua kifua, hususan wazee au wenye
magonjwa mengine sugu. Tunafanya kwa kufungua tundu dogo badala ya kupasua
kifua hivyo hupunguza hatari, maumivu na muda wa kupona,” alisema Dkt. Waane.
Alieleza kuwa katika kambi maalumu ya
matibabu hayo ya siku moja, JKCI imewafanyia upasuaji wagonjwa wawili, ikiwa ni
mara ya tatu kufanyika kwa aina hiyo ya upasuaji huku jumla ya wagonjwa tisa
wakinufaika kupitia kambi tofauti tofauti.
Kwa mujibu wa Dkt. Waane ambaye pia ni
daktari bingwa wa moyo na mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba
alisema gharama ya upasuaji huo ni kubwa kutokana na matumizi ya vifaa tiba
vinavyoagizwa kutoka nje ya nchi, ikiwemo India na Marekani, ambapo gharama ya
mgonjwa mmoja kutibiwa nje ya nchi hufikia kati ya shilingi milioni 50 hadi 90.
“Hapa nchini, serikali inachangia kati
ya asilimia 80 hadi 90 ya gharama za matibabu haya kupitia mfuko wa tiba bobezi
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan hivyo
kuwawezesha wananchi wengi kupata huduma hizi bila kusafiri nje ya nchi,”
aliongeza.
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha
Magonjwa ya Moyo kwa watu wazima wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo Dkt.
George Longopa alisema faida kubwa ya upasuaji huo ni mgonjwa kutopata kovu
kifuani pamoja na kuimarika kwa ufanisi wa valvu mpya inayowekwa.
“Hapo awali kwa wagonjwa wa aina hii tulikuwa
tukifanya upasuaji wa kufungua kifua, lakini sasa tunafanya bila kufungua
kifua. Hii ni kambi ya tatu na tayari wataalamu wetu wa ndani wamejijengea
uwezo wa kuufanya upasuaji huu wenyewe,” alisema Dkt. Longopa ambaye pia ni
mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba.
Alifafanua kuwa wagonjwa waliopatiwa huduma
hiyo ni wale waliokuwa na tatizo la kuziba kwa valvu ya kusukuma damu kutoka
moyoni, hivyo kuondolewa valvu iliyoharibika na kuwekwa valvu bandia kwa
kutumia teknolojia ya kisasa.
Katika kambi hiyo, JKCI ilishirikiana
na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka India, Nilay Patel ambaye alisema
teknolojia ya matibabu hayo inalenga zaidi wagonjwa wenye umri mkubwa ili
kupunguza madhara ya kiafya yanayoweza kujitokeza.
“Nimefurahishwa sana na ubora wa
wataalamu wa JKCI pamoja na vifaa vya kisasa walivyonavyo. Hii ni Taasisi ya
mfano Afrika Mashariki,” alisema Dkt. Patel ambaye pia ni mtaalamu wa kuzibua
mishipa ya damu ya moyo iliyoziba.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Cardimed
Africa, Nelly Otenyo alisema kampuni yake imeendelea kushirikiana na JKCI tangu
mwaka 2017 katika kusambaza vifaa tiba vinavyotumika kwenye upasuaji huo wa
TAVI.
“Tunaona fahari kuona madaktari wa
ndani sasa wana uwezo wa kufanya upasuaji huu hapa nchini. Zamani wagonjwa
walilazimika kwenda nje ya nchi kwa gharama kubwa, lakini sasa huduma hizi
zinapatikana ndani ya Tanzania,” alisema Otenyo.
Upasuaji wa TAVI unatajwa kuwa mkombozi mkubwa kwa wagonjwa wa moyo, hususan wazee, na ni ushahidi wa uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa na serikali katika kuboresha huduma za afya za kibingwa nchini.



Comments
Post a Comment