Rais Dkt. Samia aipongeza JKCI kwa kuwafuata wananchi mahali walipo
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi wa Taasisi, Mashirika ya Umma na Kampuni ambazo Serikali ina hisa wakati wa hafla ya kupokea gawio na michango iliyofanyika jana Ikulu jijini Dar es Salaam.
***********************************************************************************************************************************************************************************
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameipongeza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kutoa huduma ya upimaji na matibabu ya magonjwa ya moyo bila malipo kwa kuwafuata wananchi mahali walipo.
Pongezi hizo amezitoa jana wakati wa hafla ya kupokea gawio
na michango kutoka kwa Taasisi, Mashirika ya Umma na Kampuni ambazo Serikali ina hisa iliyofanyika
Ikulu jijini Dar es Salaam.
Mhe. Rais Dkt. Samia alisema taasisi ambazo zinatoa huduma ya
kuisaidia jamii kama ambavyo JKCI inafanya zinatakiwa kupongezwa na kutambuliwa
kwa mchango wao wanaoutoa.
“Taasisi ambazo zinatoa mchango wao kwa jamii kutokana na
huduma wanazozitoa nazo zinatakiwa
kuonekana na kuonesha wanachangia kiasi gani kwa umma kama ambavyo wanafanya
JKCI kwani mchango wa JKCI ni mkubwa na unaifikia jamii”, alisema Mhe. Rais
Dkt. Samia.
Kwa upande wake Msajili wa Hazina Nehemiah Mchechu alisema Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imetoa gawio la shilingi Bilioni 2 kupitia huduma
za uchunguzi na matibabu ya moyo kwa wananchi 27,600 katika mikoa 16 nchini.
Mchechu alisema kupitia jukwaa la kutathmini, kutafakari,
kusherehekea mafanikio, kusisitiza uwekezaji na uwajibikaji katika utumishi wa
umma wameona umuhimu wa kuitambua Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
kutokana na mchango wake katika jamii kupitia kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia
Suluhu Hassan tiba mkoba.
“JKCI hata tusipowasoma kwenye pesa tunawasoma kwenye
mafanikio yao, huduma ya tiba mkoba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wanayoifanya
tumeshuhudia imefika katika mikoa 16 ambapo watu 27,600 wameweza kupata huduma
za uchunguzi na matibabu ya moyo”, alisema Mchechu.
Aidha Mchechu alisema kwa mara ya kwanza JKCI imeonekana ikitoa huduma katika Kliniki zake zilizopo nje
ya makao makuu, hali inayoonyesha mafanikio na ukuaji mkubwa wa Taasisi hiyo
nchini.
“Sasa hivi ukitaka kutibiwa JKCI unaweza kwenda kwenye matawi
yake yaliyopo Oysterbay, Kawe, Dar Group Hospitali na tawi lake lingine lililopo
Arusha AICC”, alisema Mchechu”, alisema Mchechu.
Mchechu alisema kama Ofisi ya Msajili wa Hazina itaangalia namna ya kuhakikisha mafanikio na ukuaji wa biashara unaofanywa na JKCI unarudi na kuwagusa watendaji wa Taasisi hiyo ili kulete chachu kwa watu wengine kufanya kazi kwa bidii, kugusa watu wengine na mwisho waweze kugusa maisha yao.
Comments
Post a Comment