Viongozi wa JKCI watakiwa kuulinda utamaduni wao wa kuwahudumia wagonjwa


Viongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakiwa katika picha ya pamoja jana na Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Mhe. Nickson Simon mara baada ya kufungua mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo wa jinsi ya kutekeleza majukumu yao ya kazi viongozi wa taasisi hiyo yanayofanyika katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere iliyopo wilayani humo.





**************************************************************************************************************************************************************************************************
Viongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kuulinda utamaduni wa taasisi hiyo wa kuwahudumia wagonjwa kwa kiwango cha juu cha uadilifu na weledi kwa kufanya hivyo watu wengi zaidi watafaidika na huduma wanazizitoa.
Rai hiyo imetolewa jana na Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Mhe. Nickson
Simon wakati akifungua mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo wa jinsi ya
kutekeleza majukumu yao ya kazi viongozi wa taasisi hiyo yanayofanyika katika
Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere iliyopo wilayani humo.
Mhe. Simon alisema utamaduni wa taasisi yoyote ile unaweza
kusababisha taasisi ikafanya kazi vizuri au ikaanguka hii inategemea na jinsi
ambavyo wanatoa huduma kwa wateja wao.
“Utamaduni wa taasisi unauona pale ambapo wafanyakazi wake
wanawapokea wateja wao na kuwahudumia ni muhimu kila mfanyakazi akafahamu
utamaduni mlionao na kuulinda kwani utamaduni wenu ukibadilika na kuwa mbaya inaweza
kusababisha tasisi ikaanguka”, alisema Mhe. Simon.
Mhe. Simon aliwapongeza viongozi hao kwa huduma bora
wanayoitoa ya kuokoa maisha ya kwa wagonjwa wa moyo wanaowatibu wa ndani na nje
ya nchi.
“Kazi mnayoifanya ni kubwa ya kuokoa maisha ya watu ninawaomba
muendelee na moyo huo huo msikate tamaa kwani wagonjwa wanawategemea muwatibu,
wapone na kuendelea na maisha yao ya kawaida”, alisema Mhe. Simon.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Dkt.
Peter Kisenge alisema mafunzo hayo kwa viongozi yatawajengea uwezo wa kufanya
kazi zao kimkakati na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za matibabu kwa
kufuata miongozo na taratibu zilizopo.
Dkt. Kisenge ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo
alisema ili kuwapata viongozi wazuri ni lazima waandaliwe, wajitoe kufanya kazi kwa bidii na wawe
wazalendo kwani kila mtu akifanya kazi vizuri watafikia malengo waliyojiwekea
kuwa moja ya taasisi bora za kimataifa.
“JKCI ni moja ya taasisi kubwa Afrika Mashariki na Kati inahudumia
wagonjwa kutoka nchi zaidi ya 20, tunavyowapokea wagonjwa kutoka nchi za nje
wanafanya utalii tiba na hivyo kuiongezea nchi yetu mapato”.
“Tunaishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe.
Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa alioufanya katika taasisi
yetu kwani tuna vifaa tiba vya kisasa na wataalamu wa kutosha ambao wanatoa
huduma za kibingwa za matibabu ya moyo kwa wagonjwa”, alisema Dkt. Kisenge.
Naye Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia
alisema mada ya utaifa na uzalendo ambayo aliwafundisha viongozi hao
imewafanya waelewe umuhimu wa taasisi yao kwa ustawi wa nchi na wananchi kwani
wanaziba pengo lililokuwepo miaka ya nyuma la kuwapeleka wagonjwa wa moyo
kutibiwa nje ya nchi.
“Nimewakumbusha kuilinda misingi ya utaifa na uzalendo ambayo
inawaongoza katika utumishi wa umma kwani
vitu hivi viwili ndivyo vilivyoifanya
nchi yetu kuwa na amani na usalama”, alisema Kanali Mstaafu Simbakalia.
Nao viongozi walioshiriki katika mafunzo hayo walishukuru kwa
kupata nafasi hiyo na kusema kuwa yale waliyojifunza watakwenda kuyafanyia kazi
ili kuboresha huduma wanazozitoa kwa wananchi.
“Mafunzo niliyoyapata ni mazuri yatanisaidia katika utendaji
wa kazi zangu za kila siku, kama kiongozi ninajukumu la kusimamia dira ya
taasisi yetu ili itambulike kimataifa katika kutoa huduma, mafunzo na utafiti
wa moyo”alisema Dkt. Tulizo Shemu Mkururugenzi wa Hospitali ya JKCI Dar Group.
“Ili tuweze kutoa huduma bora kwa wagonjwa tunahitaji kuwa na
timu imara na yenye nguvu na kufanya kazi kwa pamoja na ushirikiano, ninaamini
haya tunayojifunza leo yataongeza ufanisi katika kazi zetu za kila siku”, alisema
Dkt. Angela Muhozya Mkurugenzi wa Upasuaji.
Dkt. Angela alisema wamefundishwa jinsi ya kuwa wazalendo kwa
nchi yao na wagonjwa wanaowahudumia na kutumia vizuri rasilimali za Serikali.
Comments
Post a Comment