Wananchi wahimizwa kuchangia matibabu ya watoto wenye magonjwa ya mo


Mjumbe wa Taasisi isiyo ya Kiserikali ya Heart Team Africa Foundation (HTAF) Irene Mbonde akiwakabidhi bidhaa zinazouzwa na Taasisi hiyo wadau waliochangia matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam.

Na: JKCI

********************************************************************************************************

Wananchi wamehimizwa kujitokeza kuchangia gharama za matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Rai hiyo imetolewa leo na mjumbe wa Taasisi isiyo ya kiserikali ya Heart Team Africa Foundation (HTAF) Irene Mbonde wakati wa maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa.

Irene alisema Taasisi hiyo ni mara yake ya kwanza kushiriki katika maonesho ya Sabasaba wakiwa na lengo la kuitambulisha taasisi hiyo katika jamii pamoja na kukusanya fedha za matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo.

“Hadi sasa kupitia maonesho haya tumeshakusanya shilingi Milioni 1,566,400/= kwaajili ya kuchangia matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)”, alisema Irene

Irene alisema sambamba na fedha hizo pia amejitokeza mdau mmoja ambeye ameahidi kuchangia gharama za matibabu kwa watoto 10 wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa na JKCI baada ya kumalizika kwa maonesho hayo.

Irene alisema mwitikio wa kuchangia matibabu ya moyo kwa watoto umekuwa mzuri kwani kila anayefika katika banda hilo anaguswa kuchangia na kwa wale ambao hawakuwa wamejiandaa wameahidi kushiriki kuchangia kwa wakati mwingine.

“Uchangiaji wa matibabu ya moyo kwa watoto unaofanywa katika banda letu ni pamoja na kununua bidhaa mbalimbali tulizonazo na wengine wamekuwa wakichangia fedha taslim”,

“Tunaendelea kuwakaribisha watu wengine ambao hawajafika katika banda letu kututembelea na kuendelea kuwachangia watoto wenye magonjwa ya moyo ambao wanatoka katika familia zisizokuwa na uwezo wa kugharamia matibabu yao”, alisema Irene

Kwa upande wake mdau aliyechangia fedha za matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo ambaye hakutaka jina lake lifahamike alisema familia nyingi za kitanzania zina uwezo wa kati hivyo wakikutana na changamoto za magonjwa makubwa kama vile ya moyo wanakuwa katika wakati mgumu na upoteza tumaini.

“Kwakweli nimefurahishwa kuiona taasisi hii inafanya jambo la kipekee kuwasaidia watoto wanaohitaji msaada wa matibabu, huu ni mfano wa kuigwa”. Alisema mdau huyo

Mdau alisema jamii inapaswa kuiunga mkono Taasisi hiyo kuhakikisha watoto wenye magonjwa ya moyo na magonjwa mengine makubwa wanaotoka katika familia duni wanapata matibabu kwa wakati na kwa urahisi.

Taasisi ya Heart Team Africa Foundation (HTAF) ni taasisi isiyo ya Kiserikali inahusika na kutafuta fedha kwaajili ya kugharamia matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotoka katika familia zisizokuwa na uwezo wa kugharmia matibabu ya moyo wanaotibiwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).  

 

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Wafanyakazi waliohama JKCI waagwa