Watu 138,699 wapata huduma za matibabu Hospitali ya Dar Group mwaka 2025

Mkurugenzi wa Hospitali ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Dkt. Tulizo Shemu akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya hospitali hiyo kwa mwaka 2025 leo wakati wa mkutano huo uliofanyika katika hospitali hiyo iliyopo Tazara jijini Dar es Salaam.



Baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group wakisikiliza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya hospitali hiyo kwa mwaka 2025 uliofanyika leo JKCI Hospitali ya Dar Group iliyopo Tazara jijini Dar es Salaam.

Na: JKCI

***********************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group imetoa huduma za upimaji na matibabu ya magonjwa mbalimbali kwa watu 138,699 kwa mwaka 2025.  

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Hospitali ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Dkt. Tulizo Shemu alisema watu wazima 124,959 na watoto 13,740 walipatiwa matibabu mwaka 2025 huku wagonjwa 4,144 kulazwa katika hospitali hiyo kwaajili ya matibabu.

Dkt. Shemu alisema ukilinganisha na mwaka 2024 Hospitali hiyo ilitoa huduma kwa wagonjwa 133,756 kati yao watu wazima walikuwa 109,931 na watoto 23,825 hivyo kuwa na ongezeko la wagonjwa 4,943 huku idadi ya watoto ikipungua na idadi ya watu wazima ikiongezeka.

“Huduma zilizotolewa kwa wagonjwa zilikuwa ni za matibabu ya moyo, matibabu ya kinywa na meno, kliniki ya magonjwa ya ngozi, matibabu ya magonjwa yanayoambukiza ikiwemo malaria, huduma za magonjwa ya dharura, kliniki ya wanawake na wajawazito, kliniki ya macho, kliniki ya pua, masikio na koo”,

“Huduma nyingine zilikuwa ni kliniki ya mfumo wa mkojo, kliniki ya magonjwa ya tumbo na ini, kliniki ya magonjwa ya figo, upasuaji mkubwa na mdogo, huduma za fiziotherapia (mazoezi tiba) na huduma za maabara”, alisema Dkt. Shemu

Aidha Dkt. Shemu alisema kwa mwaka 2025 JKCI Hospitali ya Dar Group ilitoa huduma mpya ambazo hapo awali zilikuwa hazitolewi ikiwemo kuangalia shinikizo la damu kwa masaa 24 (ambulatory blood pressure monitoring), matibabu ya kuangalia umeme wa moyo kwa masaa 24 (ECG Halter Monitoring) na kipimo cha kuchunguza mishipa ya damu ya moyo na mfumo wa umeme wa moyo katika hali ya mazoezi kwa kutumia mashine ya treadmill (Treadmill stress test).

Kwa upande mwingine Dkt. Shemu alisema watu 251 walifanyiwa uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali yakiwemo magonjwa ya moyo, ngiri, vidonda sugu, matatizo ya mifupa na mgongo pamoja na tiba ya kinywa na meno kupitia huduma za tiba mkoba zijulikanazo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services zilizofanyika katika viwanja vya Mbagala wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam.

“Kupitia kambi hiyo jumla ya watu 198 walikutwa na magonjwa mbalimbali na hivyo kupewa rufaa ya kufika JKCI Hospitali ya Dar Group kwaajili ya vipimo zaidi na kuanzishiwa matibabu”, alisema Dkt. Shemu

Dkt. Shemu alisema mwaka 2025 JKCI Hospitali ya Dar Group ilifanya upasuaji kwa wagonjwa 1,874 ikiwemo upasuaji wa mfumo wa mkojo, upasuaji wa mifupa, Upasuaji wa uzazi, Upasuaji wa pua, masikio na koo, Upasuaji wa matatizo mbalimbali ya wanawake na upasuaji wa jumla.

“Hospitali hii imeongeza urahisi wa upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi waishio Temeke, Tabata, Mbagala, Chanika, Gongo la Mboto na maeneo mengine ya ukanda huu”, alisema Dkt. Shemu

Upande wa ajira Dkt. Shemu alisema Serikali kupitia Tume ya Ajira katika Utumishi wa Umma kwa mwaka 2025 ilitoa ajira mpya kwa wafanyakazi 149 katika kada mbalimbali zikiwemo za afya, utawala, uhasibu, ugavi, ICT, na nyinginezo.


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na Burkina Faso zasaini makubaliano ya ushirikiano katika kutoa tiba ya magonjwa ya moyo

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi

Msumbiji kushirikiana na JKCI katika tiba ya moyo