Mapinduzi sekta ya Afya: JKCI yaleta teknolojia ya Roboti ya bilioni 5.5

Mtaalamu wa Maabara wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mariam Steven akiangalia hatua za upimaji wa sampuli za damu zinavyofanyika katika maabara ya kisasa ya taasisi hiyo inayotumia teknolojia ya roboti.
************************************************************************************************************************************************************************************************************************
Sekta ya afya nchini imepiga hatua kubwa kufuatia Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kuanza kutumia maabara ya kisasa yenye teknolojia ya roboti ya thamani ya shilingi bilioni 5.5 inayotarajiwa kuleta mapinduzi katika upimaji wa magonjwa mbalimbali hususan ya moyo.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini
Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge alisema maabara hiyo ni
miongoni mwa maabara kubwa na za kisasa zaidi katika ukanda wa Kusini mwa
Jangwa la Sahara ikiwa na uwezo wa kupima sampuli kwa haraka na usahihi wa hali
ya juu kwa wagonjwa wa ndani na nje ya taasisi hiyo.
Alisema uwekezaji huo mkubwa wa Serikali
umeongeza ufanisi wa huduma huku ukipunguza kwa kiasi kikubwa makosa ya
kibinadamu katika uchunguzi wa maabara.
“Maabara hii ina mifumo ya kisasa yenye uwezo
wa kutambua magonjwa hata katika hatua za awali kabisa. Pia imepunguza muda wa
kusubiri majibu ya vipimo kutoka saa tatu hadi saa moja tu”, alisema Dkt.
Kisenge.
Aliongeza kuwa teknolojia hiyo ina uwezo wa
kuchakata idadi kubwa ya sampuli kwa muda mfupi, hatua inayochangia kupunguza
muda wa mgonjwa kukaa hospitalini ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kupitia
Wizara ya Afya kuhakikisha huduma zinatolewa kwa ufanisi zaidi.
Mbali na utoaji wa huduma, Dkt. Kisenge
alisema maabara hiyo pia inatumika kama darasa hai kwa wataalamu wa afya nchini
kwaajili ya kujifunza na kubadilishana uzoefu wa kitaalamu.
Katika hatua nyingine, Dkt.Kisenge alibainisha
kuwa JKCI inaendelea kuimarisha matumizi ya teknolojia ya akiliunde (Artificial
Intelligence) ambapo mwaka 2024 walizindua mfumo wa kisasa unaowezesha
kufuatilia hali ya mgonjwa akiwa nyumbani kwa kutumia kifaa maalumu cha Dozee.
Alifafanua kuwa teknolojia hiyo hutumia shuka
maalumu ambalo huwekwa chini ya godoro la mgonjwa na kumwezesha daktari
kufuatilia viashiria muhimu vya afya ikiwemo mapigo ya moyo, upumuaji na presha
bila mgonjwa kufika hospitali.
“Tangu kuanzishwa kwa huduma hii wagonjwa
zaidi ya 100 wamenufaika. Tunatarajia kupanua zaidi matumizi ya teknolojia hii
ili kuwafikia watanzania wengi zaidi hasa walioko mbali na vituo vya huduma za
afya”, alisisitiza Dkt. Kisenge.
Mkurugenzi huyo alisema JKCI imeanzisha mfumo
wa kisasa wa kuweka miadi kwa njia ya mtandao (online booking) ambayo ilianza
kutumika mwaka 2025, ambao hadi sasa imeshahudumia wagonjwa zaidi ya 71,506.
Mfumo huo unawawezesha wagonjwa kuchagua muda wa kuonana na daktari na hivyo
kupunguza msongamano na muda wa kusubiri huduma.
Taasisi hiyo pia imeanzisha mfumo wa usajili
wa ndugu wanaotembelea wagonjwa waliolazwa (visitors management system),
unaolenga kuimarisha usalama na uratibu wa huduma wodini.
Dkt. Kisenge alieleza kuwa katika mwaka wa
fedha 2025/26, JKCI inalenga kuboresha zaidi huduma za tiba mtandao
(telecardiology) ili kupanua wigo wa huduma za kibingwa katika hospitali za
kanda na mikoa nchini.
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Maabara wa
JKCI Thadei Kavishe alisema maabara hiyo ina uwezo wa kupima zaidi ya sampuli
5,000 kwa saa moja.
“Tunapima aina mbalimbali za sampuli ikiwemo
damu, mkojo na majimaji kutoka sehemu mbalimbali za mwili kama moyo, mapafu na
tumbo”, alisema Kavishe.
Aliwataka wadau wa sekta ya afya zikiwemo hospitali
nyingine kutumia huduma za maabara hiyo kwa kuleta sampuli zao kwa uchunguzi wa
uhakika na wa kisasa.
Baadhi ya wagonjwa wanaopata huduma katika
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wameelezea kuridhishwa na maboresho ya
huduma yanayotokana na matumizi ya teknolojia ya kisasa hususan maabara ya
roboti na mifumo ya tiba mtandao.
“Zamani
nilikuwa nasubiri majibu kwa muda mrefu, lakini sasa ndani ya saa moja tayari
unapata majibu. Inasaidia sana kupunguza wasiwasi na kuanza matibabu mapema,
huduma ya maabara imekuwa ya haraka na yenye uhakika zaidi kuliko
ilivyokuwa awali”, alisema Mama Asha
Mussa mkazi wa Dar es Salaam.
“Maabara ya kisasa imeongeza imani kwa
wagonjwa kuhusu ubora wa huduma tunazozipata, unajisikia uko salama zaidi
unapojua vipimo vinafanywa kwa teknolojia ya kisasa na kwa usahihi mkubwa. Hii
inaleta matumaini makubwa kwa sisi wagonjwa wa moyo”, alisisitiza Mzee Abdallah Said mkazi wa Pwani.
Naye Neema
Joseph mkazi wa Dodoma alieleza kufurahishwa na mfumo wa kuweka miadi
kwa njia ya mtandao huku akisema umepunguza muda wa kusubiri huduma
hospitalini.
“Ninaweka miadi nikiwa nyumbani, nikifika hospitali napata huduma kwa wakati niliopanga. Hakuna tena kukaa foleni muda mrefu”, alisema Neema.


Comments
Post a Comment