Utafiti JKCI wachambua uhusiano kati ya dawa za moyo za SGLT2i na Afya ya njia ya mkojo
Utafiti mpya uliofanyika katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam umebaini kuwepo kwa ongezeko la maambukizi ya njia ya mkojo (UTI) miongoni mwa wagonjwa wa moyo wanaotumia dawa aina ya Sodium-Glucose Co-Transporter 2 Inhibitors (SGLT2i) zikiwemo dapagliflozin na empagliflozin.
Dawa hizo ambazo
zimekuwa msaada mkubwa katika matibabu ya magonjwa ya moyo na figo sasa
zinaibua mjadala mpya kufuatia kuhusishwa na hatari ya kuongezeka kwa
maambukizi ya UTI kwa baadhi ya wagonjwa.
Utafiti huo uliofanywa
na Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa JKCI Dar Group Samueli Rweyemamu kwa
kushirikiana na wataalamu wenzake na kuchapishwa katika Jarida la PLOS ONE la
nchini Marekani uliendeshwa kwa kipindi cha miezi mitatu kuanzia Machi hadi
Juni 2024. Ulihusisha jumla ya wagonjwa 141 wenye umri wa miaka 18 na kuendelea
waliokuwa wakitumia dawa za SGLT2i.
Akizungumza na
mwandishi wa habari hii jijini Dar es Salaam Dkt. Rweyemamu alisema lengo kuu
la utafiti huo lilikuwa ni kubaini kiwango cha maambukizi ya UTI, sababu
zinazochangia maambukizi hayo pamoja na uhimilivu wa vimelea dhidi ya dawa za
antibiotiki kwa wagonjwa wa moyo.
Alifafanua kuwa matokeo
ya utafiti yanaonesha kuwa kati ya sampuli 138 za mkojo zilizopimwa wagonjwa 22
sawa na asilimia 15.9 walikutwa na maambukizi ya njia ya mkojo.
“Idadi hii ni kubwa
ikilinganishwa na tafiti za awali ambazo zilionesha viwango vya chini zaidi vya
maambukizi kwa watumiaji wa dawa hizi”,
alisema Dkt. Rweyemamu.
Kwa mujibu wa utafiti
huo, vimelea vilivyobainika kusababisha maambukizi hayo kwa kiwango kikubwa ni
pamoja na Escherichia coli (asilimia 50), Klebsiella pneumoniae (asilimia
13.6), Pseudomonas aeruginosa (asilimia 9.1) na Candida spp. (asilimia 9.1).
Dkt. Rweyemamu alieleza
kuwa vimelea hivyo huathiri zaidi watu wenye kinga za mwili dhaifu wakiwemo
wagonjwa wa moyo na kisukari hali inayoongeza uwezekano wa kupata maambukizi ya
mara kwa mara.
Utafiti huo ulibaini
kuwa baadhi ya makundi yako kwenye hatari kubwa zaidi ya kupata UTI yakiwemo ya
watu wenye umri wa zaidi ya miaka 60, wanawake, pamoja na wagonjwa wanaotumia
dawa za SGLT2i kwa muda mrefu zaidi ya miezi minne.
Alibainisha kuwa sababu
kuu inayochangia hali hiyo ni glycosuria—uwepo wa sukari kwenye mkojo
unaosababishwa na matumizi ya dawa hizo. Sukari hiyo hutoa mazingira rafiki kwa
bakteria kuzaliana kwa haraka ndani ya mfumo wa mkojo na hivyo kusababisha
maambukizi yanayoweza kuwa ya kawaida kama cystitis au makali zaidi kama
pyelonephritis na urosepsis.
Kuhusu matibabu utafiti umeonesha kuwepo kwa usugu mkubwa wa
vimelea dhidi ya baadhi ya antibiotiki ikiwemo ampicillin (asilimia 100),
tetracycline (asilimia 69.2) na ceftazidime (asilimia 53.8).
Hata hivyo, dawa kama
nitrofurantoin zimeonesha ufanisi mkubwa, ambapo asilimia 84.6 ya vimelea vilionekana
kuwa nyeti huku meropenem ikionesha ufanisi wa asilimia 100.
Kutokana na hali hiyo,
Dkt. Rweyemamu ambaye pia ni Mkuu wa
Huduma za Tiba, JKCI Dar Group alisisitiza umuhimu wa wagonjwa wa moyo
kufanyiwa uchunguzi wa mkojo kabla ya kuanza tiba ili kuhakikisha wanapatiwa
dawa sahihi kulingana na aina ya maambukizi.
“Matokeo haya yanatoa
tahadhari kwa wataalamu wa afya dhidi ya matumizi ya dawa bila kuzingatia
usikivu wa vimelea, jambo ambalo linaweza kuchochea tatizo la usugu wa dawa changamoto
ambayo tayari inaongezeka katika ukanda wa Afrika Mashariki ikiwemo Tanzania”
alionya.
Utafiti huo pia umeweka
mkazo katika umuhimu wa uchunguzi wa mara kwa mara kwa wagonjwa wa moyo
wanaotumia dawa za SGLT2i, hususan kwa wazee na wanawake, ili kubaini maambukizi
mapema na kuyatibu kabla hayajawa makubwa.
Aidha, umehimiza kuimarishwa kwa sera za kitaifa za kudhibiti usugu wa viuavijasumu pamoja na kuboresha huduma za maabara nchini kwaajili ya uchunguzi sahihi wa maambukizi ya UTI.

Comments
Post a Comment