Madaktari waonya: Usisubiri dalili za Moyo zionekane ndipo uanze uchunguzi

Daktari bingwa wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Theophilly Mushi akitoa elimu ya jinsi ya kujikinga na magonjwa ya moyo kwa wafanyakazi wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) wakati wa kambi maalumu ya elimu na uchunguzi wa afya kwa wafanyakazi wa LATRA iliyofanyika jana jijini Dar es Salaam.

Afisa Muuguzi mbobezi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Happiness Muragwa akimpima kiwango cha sukari kwenye damu Afisa Mfawidhi wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) Rukia Kibwana wakati wa kambi maalumu ya kutoa elimu na uchunguzi wa afya kwa wafanyakazi wa LATRA iliyofanyika jana  jijini Dar es Salaam.

Daktari wa  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Edward Martin akitoa elimu ya magonjwa ya moyo kwa Kaimu Meneja Leseni za Usafiri wa Barabara wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) Pateli Ngereza wakati wa kambi maalumu ya kutoa elimu na uchunguzi wa afya kwa wafanyakazi wa LATRA iliyofanyika jana  katika ofisi za LATRA jijini Dar es Salaam.



Baadhi ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) wakimsikiliza daktari bingwa wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Theophilly Mushi wakati akitoa elimu ya umuhimu wa kufanya uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo mapema wakati wa zoezi la upimaji wa afya lililokuwa linatolewa kwa wafanyakazi wa LATRA jana  jijini Dar es Salaam.

Na JKCI

********************************************************************************************************

Wafanyakazi nchini wamehimizwa kujenga utamaduni wa kupima afya zao mara kwa mara ili kujua namba zao za afya na kutambua mapema viashiria muhimu vya mwili vinavyoweza kusababisha magonjwa ya moyo, shinikizo la damu na magonjwa mengine yasiyoambukiza.

Wito huo umetolewa na Daktari Bingwa wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Theophilly Mushi wakati akitoa mafunzo kwenye kambi ya upimaji wa afya kwa wafanyakazi wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) jijini Dar es Salaam.

Kambi hiyo ya upimaji na utoaji wa elimu ililenga kuongeza uelewa wa wafanyakazi hao kuhusu magonjwa ya moyo na magonjwa mengine yasiyoambukiza pamoja na namna ya kujikinga ili kuimarisha afya zao na kuongeza ufanisi katika utendaji kazi.

Akitoa elimu kuhusu magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo ya moyo Dkt. Theophilly alisema watu wengi hupata matatizo ya moyo bila kutambua dalili au chanzo chake mapema.

“Unaweza kujikuta unapata maumivu ya kifua kutokana na mbano wa mishipa inayosafirisha damu kwenda kwenye moyo kwa sababu ya mafuta mengi mwilini  hali inayoweza kusababisha ugonjwa wa mishipa ya damu ya moyo kuziba”, alisema Dkt. Theophilly.

Alifafanua kuwa kuziba kwa mishipa ya damu ya moyo kunatokana na mafuta mengi mwilini pia ni moja ya sababu kubwa ya maumivu ya kifua na matatizo ya moyo.

Dkt. Theophilly alisema baadhi ya wagonjwa wa moyo hupata changamoto ya mfumo wa umeme wa moyo ambapo mapigo ya moyo hupungua na wakati mwingine hulazimika kuwekewa kifaa maalumu cha kusaidia moyo kufanya kazi.

“Usisubiri hadi uanze kuona dalili kama kuvimba miguu, kushindwa kutembea au kupooza upande mmoja wa mwili kwani wakati huo madhara yanaweza kuwa makubwa zaidi”,  aliongeza.

Dkt. Theophilly alisisitiza umuhimu wa uchunguzi wa mapema wa afya ya moyo na kuchukua tahadhari kabla ya ugonjwa kufikia hatua ya hatari.

Kwa upande wake Afisa Uhusiano wa LATRA Mambwana Jumbe alisema wataalamu wa JKCI wamekuwa na mchango mkubwa kwa kutoa elimu ya afya kwa wafanyakazi wa mamlaka hiyo.

“Wataalamu wa JKCI wamekuja hapa LATRA na kutupatia elimu muhimu kuhusu namna ya kulinda afya ya moyo na kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza. Elimu hii ni muhimu kwa watumishi wetu”, alisema Mambwana.

Naye Afisa Leseni na Usajili wa LATRA, Denis Daudi alisema mafunzo hayo yamewasaidia wafanyazi hao kuelewa namna ya kujikinga na magonjwa yanayoathiri utendaji kazi wa mwili.

“Tumepata elimu ya kujikinga na magonjwa yanayotokana na  mtindo mbaya wa maisha na yale yasiyoambukiza yanayoathiri afya na utendaji kazi. Elimu hii itatusaidia kuchukua tahadhari mapema”,  alisema Denis.

Mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu kujikinga na magonjwa yasiyoambukiz  hususan ya moyo ili kupunguza athari zake katika jamii na maeneo ya kazi.


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na Burkina Faso zasaini makubaliano ya ushirikiano katika kutoa tiba ya magonjwa ya moyo

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi