Matumizi ya shisha na sigara kusababisha magonjwa ya moyo, matatizo ya mapafu na saratani
Vijana na wananchi kwa
ujumla wametakiwa kutunza afya zao na kujiepusha na matumizi ya tumbaku
hususani sigara na shisha yanayoweza kupelekea magonjwa ya moyo, matatizo ya mapafu
na saratani hivyo kusababisha vifo vya ghafla.
Rai hiyo imetolewa na
Mkurugenzi mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge
hivi karibuni wakati wa hafla fupi ya kuzindua taarifa ya mwaka 2025 kuhusu Kampuni za Tumbaku zinavyoingilia Sera ya
Afya nchini iliyofanywa na Chama cha Kudhibiti Tumbaku Tanzania (TTCF) katika
ukumbi wa JKCI iliyopo jijini Dar es Salaam.
Dkt. Kisenge ambaye pia
ni Daktari bingwa wa magonjwa wa moyo alisema matumizi ya tumbaku yanachangia
kwa kiasi kikubwa kusababisha vifo vya gafla vinasababishwa na madhara ya
tumbaku katika mishipa ya moyo ya damu inayopelekea magonjwa ya moyo.
“Matumizi ya tumbaku
kwa vijana hususani katika nchi za Afrika Mashariki yanaongezeka kwa kasi
ikiwemo uvutaji wa kisasa wa sigara aina ya shisha kwani kuvuta shisha mara moja
ni sawa na kuvuta sigara 100 jambo ambalo lina madhara makubwa kwenye mishipa
ya damu ya moyo inayoweza kusababisha mgando wa damu kwenye misuli ya moyo na
kusababisha vifo vya ghafla”,
“Sigara pia inaweza
kuleta madhara kwenye mapafu, kusababisha magonjwa ya saratani na kusababisha tatizo
la kiharusi hivyo wananchi hususani vijana wanatakiwa kuchukua tahadhari mapema
ili kujiepusha na madhara ya yanayosababishwa na matumizi ya tumbaku ambayo pia
huchangia katika kupunguza nguvu kazi ya taifa”, alisema Dkt. Kisenge.
Akizindua taarifa hiyo
Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Kudhibiti Tumbaku Tanzania (TTCF) Lutgard Kokulinda
Kagaruki alisema tangu mwaka 2019 Tanzania imekuwa na matumizi makubwa ya
tumbaku hali iliyosababisha nchi kuwekwa kwenye kundi la tahadhari la alama
nyekundu inayoonyesha hatari.
Lutgard alisema Serikali
iangalie namna ya kufanya marekebisho ya sheria na kupitisha muswada mpya wa
sheria ya kudhibiti tumbaku nchini utakaoisaidia jamii kutokupata madhara
yanayosababishwa na tumbaku.
“Kwa sasa sheria
inayotumika ni ya mwaka 2003 ambayo haikidhi mahitaji ya wakati huu kwani
udhaifu wake umechangia kuongezeka kwa matumizi ya tumbaku bila udhibit hali
inayosababisha madhara makubwa kiafya”, alisema Lutgard.
Kwa upande wake
Kiongozi wa Chama cha madaktari bingwa wa magonjwa ya ndani Tanzania (APHYTA)
ambaye pia ni daktari wa magonjwa ya ndani na mfumo wa upumuaji Mwanaada Kilima
alisema gharama za matibabu kwa watu wanaopata madhara yanayotokana na tumbaku
ni kubwa na madhara hayo yamekuwa yakiwaathiri vijana zaidi.
“Tunatoa rai kwa vijana
kupunguza au kuacha kabisa matumizi ya sigara na shisha kwani mgonjwa mmoja anayepata
changamoto za mfumo wa upumuaji kutokana na matumizi ya tumbaku anaweza kutumia
zaidi ya milioni nne kwa mwaka katika matibabu jambo ambalo ni hasara kwa taifa
ikilinganishwa na faida ndogo ya shilingi bilioni mbili tu inayotokana na kilimo
cha tumbaku inayopatikana nchini”, alisema Mwanaada.

Comments
Post a Comment