JKCI yawajengea uwezo viongozi katika usimamizi wa vihatarishi kwaajili ya ufanisi wa malengo
Menejimenti ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) inahudhuria mafunzo maalumu ya siku mbili
yanayolenga kuwajengea uwezo wa kutambua
na kudhibiti vihatarishi vinavyoweza kujitokeza na kuathiri taasisi hiyo katika
utoaji wa huduma bora kwa wagonjwa wanaowahudumia.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Dkt.
Peter Kisenge wakati wa ufunguzi wa
mafunzo hayo Mkuu wa Kitengo cha Sheria Adv.
Maulid Kikondo alisema ni takwa la
kisheria kwa taasisi za umma na binafsi kuwajengea uwezo viongozi wake ili
waweze kutambua na kudhibiti hatari katika maeneo yao ya kazi sambamba na
kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Adv. Kikondo alisema mafunzo hayo ni muhimu kwa viongozi katika
kulinda taasisi dhidi ya vihatarishi vinavyoweza kujitokeza ili waweze kufahamu
mbinu bora za kukabiliana navyo na kuepusha usumbufu au kusitishwa kwa huduma
za afya kwa wananchi.
“Taasisi inapokuwa na viongozi wenye uelewa wa kutosha kuhusu
usimamizi wa hatari inakuwa rahisi kupanga mikakati ya mapema ya kukabiliana na
changamoto zinazoweza kujitokeza na hivyo kuhakikisha huduma zinaendelea
kutolewa bila vikwazo”, alisema Adv. Kikondo.
Adv. Kikondo aliongeza kuwa mafunzo hayo yataisaidia JKCI
kuendelea kuwa taasisi imara na yenye uwezo wa kujibu changamoto mbalimbali kwa
wakati huku ikiweka mbele usalama wa wagonjwa, watumishi na rasilimali za
taasisi.
Kwa upande wake Mhadhiri Mwandamizi kutoka Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi
Kuu ya Morogoro Dkt. Cosmos Mbogela alisema vihatarishi hutokea wakati
wa utekelezaji wa mipango na vinaweza kusababisha taasisi kushindwa kufikia
malengo yake na hatimaye kuleta madhara.
“Mafunzo haya ni muhimu kuhuishwa kila mwaka kwani vihatarishi
vina tabia ya kubadilika. Hivyo ni muhimu kuweka mikakati ya kuhakikisha hatari
haitokei na endapo itatokea idhibitiwe mapema”, alisema Dkt. Mbogela.
Dkt. Mbogela alisema
taasisi nyingi hukumbwa na changamoto kubwa pale zinaposhindwa kutambua
vihatarishi mapema jambo ambalo huweza kuathiri utekelezaji wa majukumu yake ya
kila siku pamoja na kushusha kiwango cha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Alisisitiza kuwa usimamizi bora wa vihatarishi unahitaji
ushirikiano wa viongozi na watumishi wote ndani ya taasisi kwani kila mmoja ana
wajibu wa kubaini mapema viashiria vya hatari na kuchukua hatua stahiki kabla
madhara hayajatokea.
Nao viongozi walioshiriki katika mafunzo hayo walisema yamekuwa
yenye manufaa makubwa kwao kwani yamewapa uelewa mpana kuhusu namna ya kutambua
vihatarishi katika maeneo yao ya kazi na kuweka mikakati madhubuti ya kuvizuia
au kuvipunguza kabla havijaleta madhara.
“Mafunzo haya yatatusaidia viongozi kubaini vihatarishi na kuweka
mikakati ya kukabiliana navyo ili kuendelea kutoa huduma bora kwa wagonjwa
wanaofika katika taasisi yetu kupata huduma”.
“Hii ni fursa kwetu viongozi kuboresha maeneo yetu ya kazi kwa
manufaa ya wananchi na watu tunaowaongoza kwani ikiwa hatari itatokea na
tukashindwa kuidhibiti mapema wagonjwa wanaweza kupata madhara”, alisema Robet Mallya
Mkurugenzi wa Uuguzi.
Akielezea umuhimu wa mafunzo hayo Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi
na Ugavi, Renatha Miiruko alisema ikiwa
vihatarishi havitawekewa mikakati ya kudhibitiwa vinaweza kusababisha hasara
katika utendaji wa taasisi.
“Vihatarishi vinaweza kuipeleka taasisi katika hali isiyotarajiwa
iwapo havitachukuliwa hatua stahiki. Hivyo ni muhimu kufanyia kazi mafunzo haya
ili kusaidia kuilinda taasisi dhidi ya madhara yanayoweza kujitokeza kutokana
na kuchelewa kuchukua hatua” alisema Renatha.
CPA.
Juma Mshana ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa ndani alisema mafunzo
hayo ni msaada mkubwa kwa viongozi hao
kwani yameongeza uelewa wa namna ya kutambua maeneo yenye hatari kiutendaji na kiutawala ndani ya taasisi
uelewa huo utasaidia kuimarisha udhibiti wa ndani na kuhakikisha rasilimali za
taasisi zinatumika kwa ufanisi na kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa.
“Kitengo cha Ukaguzi wa ndani kina nafasi muhimu katika kuzuia na
kugundua mapema vihatarishi vinavyoweza kuathiri utendaji wa taasisi. Kupitia
mafunzo haya tutaweza kuboresha mbinu za ukaguzi na kufanya kazi kwa karibu
zaidi na menejimenti katika kuhakikisha uwazi, uwajibikaji na usalama wa
rasilimali za taasisi vinaimarika kwa manufaa ya utoaji bora wa huduma za
afya”, alisema CPA. Mshana.
Comments
Post a Comment