JKCI yapima Wanamichezo 482, Yatoa elimu ya aya ya Moyo
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dar Group ambaye pia ni mratibu wa magonjwa ya moyo
kwa wanamichezo Eva Wakuganda akisalimiana na Mkuu wa Chuo cha Taaluma ya
Polisi Dar es salaam (DPA) Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Dkt. Lazaro Mambosasa
wakati alipotembelea ofisini kwake kuaga na kuwasilisha ripoti ya mwenendo wa
kambi maalumu ya siku tano ya upimaji wa magonjwa ya moyo kwa wanamichezo na Askari
Polisi walioshiriki mashindano ya Dkt.
Mambosasa Cup yaliyomalizika hivi karibuni jijini Dar es Salaam.
Afisa Muuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) Dar Group Christina Yonatham akimsajili Askari Polisi wa Chuo cha
Taaluma ya Polisi Dar es salaam (DPA) wakati wa kambi maalumu ya upimaji wa
magonjwa ya moyo kwa wanamichezo na Askari Polisi walioshiriki mashindano ya Dkt. Mambosasa Cup yaliyomalizika
hivi karibuni katika Chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es salaam (DPA).
Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) Dar Group wakiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi wa Chuo cha Taaluma
ya Polisi Dar es salaam (DPA) wanaosomea kozi ya maofisa wakati wa kuhitimisha
kambi maalumu ya upimaji wa magonjwa ya moyo kwa wanamichezo na Askari Polisi
walioshiriki mashindano ya Dkt. Mambosasa Cup yaliyomalizika hivi karibuni katika
Chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es salaam (DPA).
Na JKCI
***********************************************************************************************************
Wananchi
hususan wanamichezo wametakiwa kutambua mapema dalili hatarishi za magonjwa ya
moyo ikiwemo maumivu ya kifua, kizunguzungu na kupoteza fahamu ili kuepuka
madhara makubwa yakiwemo ya vifo vya ghafla wakati wa mazoezi au mashindano.
Wito huo
umetolewa na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group ambaye pia ni Mratibu wa Magonjwa ya Moyo
kwa Wanamichezo Eva Wakuganda wakati wa kambi maalumu ya siku tano ya upimaji
iliyofanyika wakati wa mashindano ya Dkt. Mambosasa Cup yaliyomalizika hivi karibuni katika Chuo cha Taaluma
ya Polisi Dar es Salaam (DPA).
Dkt.
Wakuganda alisema zoezi hilo la upimaji wa afya limefanikiwa kuwafikia watu
wengi kwa muda mfupi wakiwemo wanamichezo na Askari Polisi walioshiriki mashindano
hayo.
“Leo ni
siku ya tano hapa DPA ambapo tumekuwa tukihudumia wanamichezo na askari Polisi katika
mashindano ya Dkt. Mambosasa Cup na tumepima jumla ya watu 482 walioshiriki
michezo mbalimbali”, alisema Dkt. Eva.
Alieleza
kuwa katika mashindano hayo wataalamu wa JKCI wametoa huduma za vipimo vya
magonjwa ya moyo pamoja na elimu kuhusu magonjwa hayo kwa wanamichezo na askari
Polisi ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza uelewa na namna ya kujikinga.
“Tumetoa
elimu kuhusu dalili hatarishi kama maumivu ya kifua, kizunguzungu, kupoteza
fahamu au uchovu uliopitiliza ambazo zinaweza kuashiria matatizo ya moyo wakati
wa michezo”, alieleza Dkt. Eva.
Aliongeza
kuwa ni muhimu kutambua dalili za magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo ya moyo mapema
ili kuzuia hatari ya matatizo ya moyo kwa wanamichezo.
“Tunashukuru
uongozi wa chou hususan Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Dkt. Lazaro Mambosasa kwa kutukaribisha na kutuwezesha kutoa
huduma hizi muhimu kwa askari na wanamichezo ili watambue afya zao mapema”,
aliongeza.
Kwa
upande wao wanafunzi wa chuo hicho walieleza kufurahishwa na huduma walizopata
na kusema zimekuwa msaada mkubwa kwao katika mazingira ya mafunzo.
“Kwa
kweli tumepata huduma nzuri sana ambazo mara nyingi ilikuwa ngumu kuzipata
tukiwa nje ya chuo. Tunaiomba JKCI iendelee kuja tena kutoa huduma hizi kwa
sababu watu wengi tumenufaika nazo”, alisema mwanafunzi wa Chuo cha Taaluma ya Polisi
Dar es Salaam (DPA) Simula Maregesi.
“Tumepimwa vipimo mbalimbali ikiwemo moyo,
presha na sukari, tumefurahi sana kupata huduma hii. Kujua afya zetu
kutatusaidia kuendelea vizuri na mafunzo yetu hapa chuoni”, alisema Blandina
Kasongwa.
Utoaji wa
huduma hizo unaonesha umuhimu wa kuendelea kutoa elimu ya afya ya moyo kwa
makundi maalumu hasa wanamichezo ili kupunguza hatari ya matukio ya dharura
yanayoweza kuzuilika.



Comments
Post a Comment