Wafundishwa jinsi ya kurekebisha valvu za moyo

Wataalamu wa upasuaji wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakishirikiana na wenzao kutoka Shirika la Open Heart International (OHI) la nchini Australia kumfanyia upasuaji wa kurekebisha valvu ya moyo mgonjwa mwenye matatizo ya valvu wakati wa kambi maalumu ya siku 6 inayofanyika katika taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.


Wataalamu wa upasuaji wa moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakimfanyia upasuaji wa moyo mtoto mwenye tatizo la moyo wakati wa kambi maalumu ya siku 6 inayofanywa na wataalamu wa JKCI kwakushirikiana na wenzao kutoka Shirika la Open Heart International (OHI) la nchini Australia. Jumla ya watoto 10 kufanyiwa upasuaji katika kambi hiyo.

Na: JKCI

*******************************************************************************************************

Wataalamu wa upasuaji wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wanapewa mafunzo ya kutibu valvu za moyo kwa kuzirekebisha badala ya kuzitoa na kuweka valvu za bandia.

Mafunzo hayo yanatolewa na wataalamu wa afya kutoka Shirika la Open Heart International la nchini Australia kwa kipindi cha wiki moja wakati wa kambi maalumu inayoendelea JKCI lengo likiwa kuwapa muda wagonjwa wenye changamoto za valvu kujenga familia zao kabla ya valvu zao kubadilishwa.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Upasuaji wa Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya alisema kambi hiyo ni maalumu kwaajili ya kujifunza na kuongeza ujuzi kwa wataalamu wa upasuaji wa moyo wa JKCI.

Dkt. Angela alisema kwa kawaida mgonjwa akishabadilishiwa valvu za moyo anatakiwa kutumia dawa za kuzuia kugandisha damu katika  maisha yake yote, lakini kama wakizirekebisha inawasaidia kutotumia dawa mapema na kwa wanawake inawapa muda ya kutengeneza familia zao na baadaye hubadilishiwa.

“Sasa hivi kuna wimbi kubwa la watoto wenye umri kati ya miaka 15 hadi 20 wanapata matatizo ya lavlu za moyo kuchoka na kuhitajika kubadilishiwa valvu, tumefanya kambi hii kuwasaidia wagojwa kurekebisha valvu zao”,

“Wanawake ambao valvu zao za moyo zimechoka na kuwekewa valvu bandia inawazuia kubeba ujauzito kutokana na dawa wanazotakiwa kutumia katika maisha yao yote lakini kama tutazirekebisha tutakuwa tumewapa muda wa kujenga familia zao kwanza na baada ya muda ndio zitabadilishwa”, alisema Dkt. Angela

Kwa upande wake Daktari kutoka Shirika la Open Heart International la nchini Australia Dareen Wolfers alisema wataalamu wa afya kutoka shirika hilo wamekuwa wakishirikiana na wataalamu wa JKCI toka mwaka 2015 ambapo kwa sasa wanaiona taasisi hiyo kuwa taasisi bora Afrika katika kutoa huduma za matibabu ya moyo.

Dkt. Wolfers alisema katika kambi hii wamekuja kwaajili ya kuongeza ujuzi kwa wataalamu wote wanaomhudumia mgonjwa aliyefanyiwa upasuaji wa moyo hivyo kuleta wataalamu wa upasuaji, wataalamu wa usingizi, madaktari na wauguzi wa chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU) cha wagonjwa waliofanyiwa upasuaji wa moyo.

“Katika kambi hii tutawafanyia upasuaji wa moyo watoto kati ya 8 hadi 10 na watu wazima kati ya 5 hadi 8 kwani kambi hii ni kwaajili ya kujifunza Zaidi”, alisema Dkt. Wolfers

Naye afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) anayepata mafunzo kupitia kambi hiyo Lilian Peter alisema mafunzo anayopata yanamsaidia kuweza kutambua kwa haraka changamoto anazopitia mgonjwa na kuweza kumsaidia.

Lilian alisema ameanza kufanya kazi za kuhudumia katika chumba cha wagonjwa wa dharura na mahututi (ICU) tangu mwaka 2019, ujuzi anaoupata kutoka kwa wataalamu hao unazidi kumpa uwezo wa kuokoa maisha ya wagonjwa hao.

“Kupitia mafunzo haya naweza kusimama mwenyewe, nikamuhudumia mgonjwa na kutambua matatizo ambayo mgonjwa anayapata na kumsaidia kwa wakati”, alisema Lilian

Lilian alisema baada ya yeye kupata mafunzo hayo atawasaidia wataalamu wengine wa afya kuweza kutoa huduma kwa wagonjwa wa dharura na mahututi ili kwapamoja waweze kuokoa maisha.


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)