Wasanii waishukuru JKCI kwa kuwapa huduma za matibabu ya moyo


Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Kliniki ya Kawe Nicholaus Steven akizungumza na mwananchi aliyefika katika kliniki hiyo iliyopo jengo la Mkapa Health Plaza barabara ya Tuari jijini Dar es Salaam kwaajili ya kupata huduma za upimaji na matibabu ya moyo.


Wananchi waliofika katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Kliniki ya Kawe wakisoma taarifa mbalimbali zinazohusiana na taasisi hiyo wakati wakisubiri kupatiwa huduma.

Picha na: Khamis Mussa

**************************************************************************************************************

Na Khamisi Mussa - Dar es Salaam

Wasanii waishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kuwapa huduma za uchunguzi, matibabu ya moyo pamoja na elimu ya namna ya kujikinga na magonjwa hayo.

Huduma hiyo inafanyika katika Kliniki ya JKCI iliyopo Kawe jengo la Mkapa Hearth Plaza barabara ya Tuari imelenga kuyafikia makundi ya wasanii na wanamichezo kwa kuwapa huduma bila gharama kila jumamosi na jumapili kwa kipindi chote cha mwezi Desemba.

Akizungumza na mwandishi wa habari hii muigizaji kutoka bongo movie Khadija Kizito alisema akiwa kama msanii ambaye ni kioo cha jamii ameona ni muhimu kuwa mfano kwa wengine kujitokeza kupima afya yake kutokana na maradhi yasiyoambukiza kuongezeka kwa kasi.

Khadija alisema baada ya kupata taarifa ya upimaji wa magonjwa ya moyo kwa wasanii kutoka kwa viongozi wake na kutokana na alivyokuwa akijisikia akaona atumie fursa hiyo kufika JKCI kupima afya yake.

“Nawashukuru sana viongozi wangu akiwemo Stive Mengele pamoja na mama Hidaya Njaidi ambao wameweza kutufanikishia sisi wasanii kuweza kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo”, alisema Khadija

Aidha Khadija amewakumbusha wasanii wenzangu kujitokeza kwa wingi kufanya uchunguzi wa magonjwa ya moyo ili waweze kuchukua hatua mapema kwani pamoja na kupata elimu sahihi kutoka kwa wataalamu wa JKCI.

“Nawashukuru sana wataalamu wa JKCI nimepokelewa vizuri, nimefika hapa nikiwa sijisikii vizuri lakini baada ya mapokezi mazuri hata hali yangu ikaanza kuwa na nafuu”, alisema Khadija

Kwa upande wake Salma Kanige ambaye ni mkazi wa Kawe ameipongeza Serikali ya awamu sita kwa kujali afya za wananchi wake na kuwasogezea huduma karibu na wanapoishi.

Salma alisema hapo awali matibabu ya moyo yalivyokuwa yakitolewa eneo la upanga ilikuwa inawapa watu uvivu kuamka na kwenda upanga kwaajili ya kuchunguza afya lakini baada ya huduma hizo kusogezwa Kawe inakuwa rahisi mtu kufika na kuchunguza afya yake.

“Kwakweli Serikali hii imeona umuhimu wa kupeleka huduma karibu na wananchi kwakutuongezea kituo hiki cha Kawe, zamani tulikuwa hatuendi kufanya uchunguzi tulikuwa tunasubiri hadi tuumwe ndio tunaenda hospitali kwasababu upanga ilikuwa mbali”, alisema Salma


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)