21 wafanyiwa upasuaji wa moyo ndani ya siku tano


 Madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao kutoka Shirika la Cardiostart International la nchini Marekani na Uingereza wakimfanyai upasuaji  mgonjwa ambaye valvu yake  ya upande wa kushoto imebana kiasi cha kushindwa kupeleka damu katika mfumo wa mwili, mgonjwa huyu amewekewa valvu ya chuma (mechanical valve) ambayo  itasaidia kupeleka damu kwenye mfumo  wa mwili mzima. Upasuaji huo umefanyika  katika kambi maalumu ya matibabu ya siku tano ambapo wagonjwa 11 walipata matibabu.

Wataalamu wa upasuaji wa moyo kwa watoto  kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na mwenzao kutoka nchini Ujerumani Benjamin  Bierbach wakimfanyia upasuaji mtoto aliyezaliwa na mshipa mmoja badala ya miwili unaotoa damu kwenye moyo (Truncus Arteriosus),mtoto huyo alifanyiwa upasuaji wa kutengeneza mshipa mmoja wa kupeleka damu kwenye mwili (Aorta) na mwingine kupeleka damu kwenye mapafu (Pulmonary Artery). Upasuaji huo umefanyika katika kambi maalum ya siku tano ya upasuaji wa moyo ambapo watoto 10 walitibiwa.

Picha na Khamisi Mussa

*************************************************************************************************************************************************************************************************************************************

Wagonjwa 21 wenye matatizo ya moyo wakiwemo watoto  na watu wazima wamefanyiwa upasuaji katika kambi maalum za matibabu ya moyo zilizomalizika  jana katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es Salaam.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Upasuaji wa moyo Dkt. Angela Muhozya wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kambo hizo mbili za upasuaji.

Dkt. Angela ambaye pia ni daktari bingwa wa  usingizi na wagonjwa mahututi alisema kwa muda wa siku tano katika Taasisi hiyo kulikuwa na kambi mbili za matibabu ambapo  wagonjwa 21 walifanyiwa upasuaji.

Alisema watoto 10 walifanyiwa upasuaji na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na mwenzao kutoka nchini Ujerumani ambapo watu wazima 11 walifanyiwa upasuaji na wataalamu wa Taasisi hiyo kwa kushirikiana na wenzao wa Shirika la Cardiostart International.

“Wiki hii tumekuwa na kambi za kimatibabu mbili tofauti moja kwa watoto na nyingine ni kwa watu wazima. Katika kambi ya watu wazima tumekuwa na wataalamu kutoka Shirika la Cardiostart International ambalo ni mchanganyiko wa madaktari kutoka nchini Uingereza na Marekani tumewapandikiza wagonjwa mishipa ya damu na kubadilisha valvu kwa wagonjwa ambao valvu zao ziliharibika kabisa,”.

 “Wataalamu wetu wa magonjwa ya moyo kwa watoto kwa kushirikiana na mwenzao Benjamin kutoka nchini Ujerumani walifanya upasuaji kwa watoto ambao mishipa yao ya damu, valvu pamoja na vyumba vya moyo vilikuwa na matatizo,”.

 “Wagonjwa wote waliofanyiwa upasuaji wanaendelea vizuri na wengine wameshatoka katika chumba cha uangalizi maalum (ICU) na kwenda wodini kwa ajili ya kuanza mazoezi pamoja na kuendelea na matibabu mengine,” alisema Dkt. Angela.

Dkt.Angela alisema upasuaji huo uliofanywa na madaktari hao ni ule mgumu, ambao ungewalazimu wagonjwa hao kusafirishwa ili kutibiwa nje ya nchi.Upasuaji huo umefanyika kwa wagonjwa ambao mioyo yao ilikuwa inafanya kazi chini ya asilimia 25, hivyo walilazimika kubadilishiwa valvu za moyo ambazo zilikuwa zimeharibika sana  na hasa kwa watu wazima sana.

 Alisema gharama za matibabu haya yote katika Taasisi hiyo ni milioni 250 ambapo fedha hizo zimelipwa kwa bima za afya, wagonjwa wamelipia na pia kuna wagonjwa ambao wamepata msamaha wa matibabu lakini kama wagonjwa hao wangetibiwa nje ya nchi Serikali ingelipa zaidi ya shilingi milioni 525.

Alimshuku  Dkt.Benjamin Bierbach kutoka Ujerumani ambaye alikabidhi vifaa maalumu vyenye thamani ya shilingi  bilioni 2, ambavyo vimesaidia katika kufanikisha upasuaji kwa watoto  waliozaliwa na mshipa mmoja mkubwa unaounganika kutoka katika vyumba viwili vya moyo.

Naye Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto kutoka JKCI Godwin Sharau alisema wiki hii wamekuwa na Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto  kutoka nchini  Ujerumani Benjamin Bierbach ambapo watoto 10 ambao walikuwa na matatizo ya mishipa ya damu, Valvu na vyumba vya moyo walifanyiwa upasuaji.

“Tumekuwa na Dkt Benjamin huu ni mwaka wa saba hata wakati wa UVIKO 19 Daktari huyu aliendelea kuja JKCI na kufanya matibabu kwa watoto wenye shida ya moyo,na katika kambi hii tumeshirikiana kwa pamoja kufanya upasuaji kwa watoto ambao wamezaliwa na matatizo ya Valvu, vyumba vya moyo na mishipa ya damu tumewapandikizia mishipa ya bandia ambayo watakaa nao kwa muda wa miaka kumi na tano na watabadilishiwa mingine,”.

“Dkt Benjamini pamoja na kuja kufanya upasuaji wa watoto pia amekuja na mishipa ya bandia ambayo ndiyo iliyotumika kuwawekea watoto hao,mishipa hii ni ya gharama sana na hivyo tunapopata nafasi ya kuwa na kambi kama hizi watoto wengi wanahudumiwa na pia tunaongeza uzoefu mkubwa zaidi wa kuwahudumia watoto,” alisema Dkt. Sharau.


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari