Kuwait, JKCI kuimarisha matibabu ya moyo kwa watoto
Daktari bingwa wa usingizi kutoka Shirika linalotoa msaada wa matibabu ya moyo kwa watoto la Children’s Heart Charity Association lililopo nchini Kuwait Hesham Menshawy akielezea namna ambavyo shirika hilo litashirikiana na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kutoa huduma za matibabu ya moyo kwa watoto walipotembelea JKCI leo jijini Dar es Salaam.
Daktari bingwa wa Upasuaji wa moyo kwa watoto kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Godwin Sharau akiwaelezea aina ya upasuaji wa moyo wanaoufanya kwa watoto Madaktari bingwa wa moyo kwa watoto kutoka Shirika linalotoa msaada wa matibabu ya moyo kwa watoto la Children’s Heart Charity Association lililopo nchini Kuwait walipotembelea Taasisi hiyo kwa ajili ya kuona namna ya kushirikiana na Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam.
Madaktari bingwa wa moyo kwa watoto kutoka Shirika linalotoa msaada wa matibabu ya moyo kwa watoto la Children’s Heart Charity Association lililopo nchini Kuwait wakiangalia huduma zinazotolewa katika moja ya chumba cha kliniki ya magonjwa ya moyo kwa watoto walipotembelea JKCI kwa ajili kuangalia namna ya kushirikiana na Taasisi hiyo leo jijini Dar es Salaam.
********************************************************************************************************************************************************************************
Shirika la Children’s Heart Charity Association la
nchini Kuwait linalotoa msaada wa matibabu ya moyo limepanga kuboresha huduma
za kibingwa za matibabu kwa watoto nchini kwa kushirikiana na Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI).
Licha ya huduma za kibingwa shirika hilo pia limepanga
kujenga jengo jipya la JKCI, kutoa mafunzo kwa wataalamu wa afya wa JKCI, kutoa
vifaa tiba na kuiwezesha Taasisi hiyo
kutoa huduma za upimaji na matibabu ya moyo kwa wananchi kwa kuwafuata mahali
walipo.
Watalaam wa shirika hilo walitembelea taasisi hiyo leo na kuona
watoto wanaotibiwa JKCI walifarijika kuona uwekezaji mkubwa uliofanywa na
serikali kwa ajili ya matibabu ya moyo yanayotolewa hapa nchini kwa watanzania
wenye uhitaji wa huduma hizo.
Akizungumza wakati wa ugeni huo Mkurugenzi Mtendaji wa
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema Shirika la
Children’s Heart Charity Association limeahidi kuangalia kama kutakuwa na
uwezekano wa kujenga jengo jipya la JKCI ambalo litaongeza upatikanaji wa huduma
za matibabu na upasuaji wa moyo hususani kwa watoto.
“Katika kushirikiana nasi wataalam hawa wameahidi pia
kutuletea vifaa tiba ambavyo vitatumika katika matibabu ya watoto ikiwa ni
sehemu ya kutoa huduma rafiki kwa watoto kwani watoto wengi wanatoka katika
familia zisizokuwa na uwezo wa kugharamia matibabu,” alisema Dkt. Kisenge.
Dkt. Kisenge alisema Shirika hilo pia limeahidi kushirikiana
na JKCI kutoa mafunzo kwa wataalam kwa kuwaleta wataalam wao hapa nchini
kubadilishana uzoefu na wataalam JKCI lengo likiwa ni kuifanya taasisi hiyo
kuwa bora nchini Tanzania na Afrika yote.
“Magonjwa ya moyo kwa watoto yanazidi kuongezeka hapa nchini
hivyo kuongeza uhitaji wa matibabu ya magonjwa hayo kuwa kubwa, naamini ujio wa
wataalam hawa kutoka nchini Kuwait utaenda kusaidia watoto wengi kufikiwa na
matibabu haya ya moyo,” alisema Dkt. Kisenge.
Aidha Dkt. Kisenge alisema JKCI katika mpango mkakati wake wa
kutoa huduma bora na rafiki kwa watanzania imekuwa ikiwafuata wananchi mahali walipo
ili kila mwenye uhitaji na huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo aweze kuzipata
jambo ambalo limeungwa mkono na watalaam hao kutoka Shirika la Children’s Heart
Charity kwa kuahidi kuiwezesha JKCI ili
iweze kuwafikia wananchi nchi nzima.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. William Mahalu alisema watalam wa afya kutoka
nchini Kuwait wameonesha nia ya kusaidia kutibu watoto wenye magonjwa ya moyo
nia ambayo sio kila mtu anaweza kujitoa kwa ajili ya watoto hao.
“Tumeainisha mahitaji tuliyonayo ikiwemo ucheleweshwaji wa
watoto kufikishwa hospitali kwa ajili ya matibabu hivyo kuwaomba watusaidie
vitendea kazi ambavyo zitakuwa mikoa yote hapa nchini ili tuweze kutoa huduma
za utambuzi wa magonjwa haya na kuwabaini mapema watoto wenye magonjwa ya moyo,”.
“Kwa hapa tulipo sasa tupo katika nafasi nzuri ya kutoa
huduma za matibabu ya moyo kwani zimepunguza matatizo kwa asilimia kubwa lakini
bado tunahitaji kufanikiwa zaidi hivyo tumewaomba wasichoke kubadilishana nasi
uzoefu ili tuweze kupanda zaidi katika kutoa huduma za kibingwa za matibabu ya
moyo,” alisema Prof. Mahalu.
Naye Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo wa kufungua kifua kwa watoto kutoka Shirika linalotoa msaada wa
matibabu ya moyo kwa watoto la Children’s Heart Charity Association lililopo
nchini Kuwait Faisal Al-Saiedi alisema Shirika hilo limekuwa likitoa msaada wa
matibabu kwa watoto wengi duniani na sasa likaona ni vizuri kama litawafikia
watoto wa Tanzania ili nao waweze kufaidika na msaada wa matibabu hayo.
“Natambua kuwa kuna watoto wengi wanaohitaji msaada wa
matibabu ya moyo hapa Tanzania, na wataalam wa hapa wanafanya kazi nzuri
kuwasaidia watoto hao hivyo nasi tunataka kushirikiana nao kuwasaidia watoto
hao lakini pia kuwavusha hatua moja zaidi katika kutoa huduma bora za matibabu
ya moyo kwa watoto wetu,” alisema Dkt. Faisal.
Comments
Post a Comment