Msomali aishukuru JKCI kwa upasuaji wa mtoto wake

 

Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto Evelyn Furumbe na  Afisa Muuguzi Mariam Makapu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakimuhudumia mtoto kutoka nchini Somalia ambaye amefanyiwa upasuaji wa kuzibwa tundu la moyo katika Taasisi hiyo ambaye ameruhusiwa kutoka wodini leo tarehe 07/11/2022. Kulia ni bibi wa mtoto huyo Halimo Isse.

 Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto Evelyn Furumbe na Afisa Muuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mariam Makapu wakimuhudumia mtoto kutoka nchini Somalia ambaye alifanyiwa upasuaji wa kufungua kifua na kuzibwa tundu la moyo katika Taasisi hiyo, mtoto huyo  ameruhusiwa  kutoka wodini leo tarehe 07/11/2022.

Hirs Ally ambaye ni baba mdogo wa mtoto aliyefanyiwa upasuaji wa moyo kutoka nchini Somalia akimtazama kwa furaha mtoto huyo mara baada ya kuruhusiwa kutoka wodini katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) alikokuwa anapatiwa matibabu.

*******************************************************************************************************************************************************************************************************************

Raia wa Somalia ameshukuru kwa huduma ya upasuaji wa kuziba tundu la moyo aliofanyiwa mtoto wake mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi miwili katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Shukrani hizo amezitoa leo jijini Dar es Salaam wakati akiongea na mwandishi wa habari hizi mara baada ya mtoto huyo kuruhusiwa kutoka wodini ambako alikuwa anapatiwa matibabu.

Hirs Ally ambaye ni baba mdogo wa mtoto alisema baba wa mtoto huyo aliyeko nchini Somalia alipata taarifa ya kupatikana kwa huduma ya upasuaji wa moyo JKCI na hivyo kumtuma mtoto huyo aliyeambatana na  bibi yake kuja hapa nchini kwa ajili ya kupatiwa matibabu.

“Tunashukuru huduma tuliyoipata ni nzuri kuna vifaa vya kutosha pia madaktari na wauguzi ni marafiki kila unachowauliza wanakujibu na wanakwambia kila kitu ambacho mtoto anaenda kufanyiwa,”.

“Tuliamua kumleta mtoto wetu JKCI kwani gharama za matibabu ni ndogo ukilinganisha na nchini Somalia pia kuna wataalamu wenye ujuzi wa hali ya juu na vifaa viko vya kutosha, ninawasihi wazazi wenye watoto ambao wanamatatizo ya moyo wawalete hapa kwa ajili ya matibabu,”alisema Hirs.

Kwa upande wake daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Evelyn Furumbe alisema walimpokea mtoto huyo mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi miwili tarehe 10/10/2022 na baada ya kumfanyia vipimo waligundua moyo wake una tundu.

Dkt. Evelyn alisema tarehe 11/10/2022 mtoto alifanyiwa upasuaji wa kuziba tundu hilo ambapo hadi sasa anaendelea vizuri na leo hii ameruhusiwa na atarudi kwa ajili ya kliniki baada ya wiki mbili ili kuangalia maendeleo yake.

“Mtoto alikuwa na tundu ambalo linakuwa kati ya mshipa wa kupeleka damu kwenye mwili (Aorta) na wa kupeleka damu kwenye mapafu (Pulmonary) hili tundu mtoto akizaliwa huwa linafunga lakini la kwake halikufunga na lilikuwa na ukubwa wa milimita 6. Pia alikuwa na nyama chini ya Valvu ambayo ilikuwa inasababisha damu kupita kwa kasi katika Aorta na kusababisha mlango wa Aorta kuharibika na kuanza kuvuja damu hivyo basi tiba yake ilikuwa ni  kukata nyama na kuziba  tundu,”.

“Watoto wenye shida kama hizi huwa tunawapokea mara kwa mara na wanafanyiwa upasuaji na kupona na kuendelea na maisha kama watoto wengine,” alisema Dkt. Evelyn.


 

 


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari