JKCI kushirikiana na Poland kutibu magonjwa ya moyo
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imesaini mkataba na
chuo Kikuu cha Jagiellonian kilichopo nchini Poland kwa ajili ya kushirikiana
katika kubadilishana ujuzi wa kutoa huduma za kibingwa za matibabu na upasuaji
wa moyo.
Mkataba huo ambao utaanza kutumika mapema mwakani ulisainiwa jana
jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) Dkt. Peter Kisenge na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Jagiellonian cha
nchini Poland Prof. Bartlomiej Guzik.
Akizungumza na waandishi wa habari hizi Dkt. Kisenge alisema
JKCI imesaini mkataba na chuo hicho ili kuweka ushirikiano ambao umelenga
kuongeza wigo katika kutoa tiba ya magonjwa ya moyo pamoja na upasuaji wa moyo
katika Taasisi hiyo.
“Tumesaini makubaliano ambayo yatawawezesha wataalam wetu
kwenda nchini Poland kwa ajili ya kujifunza namna wenzetu wanavyotoa huduma za
matibabu ya moyo lakini wao pia watakuja hapa kwetu kuona na kujifunza jinsi
tunavyotoa huduma za tiba na upasuaji wa moyo”,
“katika ushirikiano huu pia tumekubaliana wenzetu hawa
watatuletea wataalam ambao watashirikiana nasi katika kuwahudumia wagonjwa kwa
kufanya matibabu ya kibingwa ya upasuaji wa moyo hasa kuzibua mishipa ya damu
ambayo imeziba, kubadilisha valvu za moyo bila kupasua kifua upasuaji unaoitwa TAVI procedure ambao kwa hapa nchini
kwetu bado haujaanza kufanyika”, alisema Dkt. Kisenge
Dkt. Kisenge alisema JKCI imeongeza wigo wa kuwa na ushirikiano
na mashirika yanayotoa huduma za kibingwa za matibabu ya moyo kutoka nchi 18 ikiwemo
nchi hiyo ya Poland ambayo itaanza rasmi kubadilishana ujuzi na wataalam wa
Taasisi hiyo mapema mwakani.
“Tutaendelea kuongeza ushirikiano huu wa kubadilishana uzoefu
na nchi nyingine ambazo tunaamini zinatoa huduma za kibingwa za matibabu ya
moyo nia ikiwa ni kuifanya JKCI kutoa matibabu ya kibingwa ya magonjwa ya moyo
katika Afrika yote”, alisema Dkt. Kisenge
Naye Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Jagiellonian kilichopo
nchini Poland Prof. Bartlomiej Guzik alisema wamevutiwa kufanya kazi na
wataalam wa afya wa JKCI ili kwa pamoja waweze kutoa huduma za kibingwa za
matibabu na upasuaji wa moyo kwa wagonjwa wanaohitaji huduma hiyo.
“Kujenga uhusiano baina yetu na JKCI kutasaidia kuboresha
huduma za kibingwa za matibabu na upasuaji wa moyo lakini pia kutaongeza
ubobezi kwa wataalam hawa wa afya”, alisema Prof. Bartlomiej.
Comments
Post a Comment