Wananchi wa Geita tafuteni tiba sahihi kwa wataalam wa afya – Mhe. Martha Mkupasi

Mkuu wa Wilaya ya Chato Mhe. Martha Mkupasi, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Pro. William Mahalu, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge na Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato (CZRH) Dkt. Brian Mawalla wakikata utepe kuashiria uzinduzi wa kliniki ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo wakati wa ufunguzi wa kambi maalum ya matibabu ya moyo inayofanywa na madaktari wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa CZRH leo katika Hospitali hiyo iliyopo Wilaya ya Chato


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na wananchi wa mkoa wa Geita waliofika katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato (CZRH) kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi na matibabu ya moyo wakati wa ufunguzi wa kambi maalum ya siku tano inayoendelea katika Hospitali hiyo iliyopo Wilaya ya Chato.


Mkuu wa Wilaya ya Chato Mhe. Martha Mkupasi akizungumza na baadhi ya wananchi wa Mkoa wa Geita waliofika katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato (CZRH) kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi na matibabu ya moyo wakati wa ufunguzi wa kambi maalum ya siku tano ya matibabu ya moyo inayoendelea katika Hospitali hiyo iliyopo Wilaya ya Chato.


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimwelezea Mkuu wa Wilaya ya Chato Mhe. Martha Mkupasi umuhimu wa kipimo cha kuchunguza jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiograph – ECHO) wakati wa ufunguzi wa kambi maalum ya siku tano ya matibabu ya moyo inayoendelea katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato iliyopo Wilaya ya Chato.


Mkuu wa Wilaya ya Chato Mhe. Martha Mkupasi akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Prof. William Mahalu na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge pamoja na viongozi na wataalam wa afya wa JKCI na wenzao wa CZRH wakati wa ufunguzi wa kambi maalum ya siku tano ya matibabu ya moyo inayoendelea katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato iliyopo Wilaya ya Chato.

 Na: JKCI

**************************************************************************************

Wananchi wa Mkoa wa Geita na mikoa ya jirani wametakiwa kufuata huduma za matibabu hospitali pindi wanapojisikia kuumwa ili waweze kupata tiba halisi na kuondoa fikra potofu za kufuata tiba hisia zinazotolewa na watu ambao sio wataalam wa afya.

Rai hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Wilaya ya Chato Mhe. Martha Mkupasi wakati wa uzinduzi wa kambi maalum ya matibabu ya moyo ya siku tano inayofanywa na wataalam wa afya kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato (CZRH) inayoendelea katika Hospitali hiyo.

Mhe. Martha alisema kuwa lengo la serikali ni kusogeza huduma karibu zaidi kwa wananchi pamoja na kuwapunguzia gharama za kufuata huduma za matibabu mbali ya makazi yao ndio maana leo hii Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato inajengewa uwezo ili nayo iwe sehemu ya kusogeza huduma na kupunguza gharama kwa wananchi wa Mkoa wa Geita.

“Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Chato imewekezwa vifaa vyote vya matibabu ya moyo vyenye gharama kubwa hivyo nawaomba wananchi wote mtakaposikia dalili za kuumwa mfike katika Hospitali hii ili muweze kupata tiba halisi muache kwenda kwenye tiba hisia”, alisema Mhe. Martha

Mhe. Martha alisema kuwa ujenzi wa CZRH ulianza awamu ya tano ambapo Mhe. Rais wa awamu ya sita mama Samia Suluhu Hassan aliahidi kuhakikisha miradi yote iliyoanza awamu ya tano inakamilika na inafanya kazi kwa asilimia 100 jambo ambalo linathibitishwa leo katika Hospitali hiyo ya Rufaa ya Kanda Chato.

 “Nawaomba wataalam wa afya wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato kuweka jitihada ya pekee kupokea yale wanayofundishwa na wataalam wa afya kutoka JKCI ili baada ya kambi hii muweze kuwahudumia na kuwapatia matibabu wananchi wa Chato, mikoa ya jirani pamoja na nchi zilizopo jirani na Chato”,

“Nawashukuru watumishi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo ambao hawakuona umbali wa Wilaya yetu ilipo bali wao walidhamiria kuja kutoa huduma za matibabu ya moyo na kuleta faraja kwetu sisi wananchi wa kanda ya ziwa”, alisema Mhe. Martha

Akizungumzia kambi hiyo ya uchunguzi na matibabu ya moyo Mwenyekiti wa bodi ya wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Prof. William Mahalu alisema kuwa wataalam wa afya wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato wamekua na utayari wa kupokea ujuzi unaotolewa na watalaam wa JKCI kwa kuwa mstari wa mbele kufanya kazi kwa pamoja na wataalam hao jambo ambalo linatoa motisha ya kuendelea kuwajengea uwezo.

Prof. Mahalu alisema kuwa jitihada zinazofanywa na wataalam wa afya wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato kama zitaendelezwa kwa kujengewa uwezo mara kwa mara na kupelekwa masomoni kwa ajili ya kuwa wataalam wabobezi wa magonjwa ya moyo kutaifanya hospitali hiyo kuwa hospitali bingwa ya magonjwa moyo nchini na kupunguza idadi ya wagonjwa wanaopelekwa nje ya nchi kwa ajili ya matibabu

“Nilivoteuliwa na Rais wa awamu ya tano kuwa mwenyekiti wa bodi ya wadhamini ya JKCI nilipewa agizo la kupunguza idadi ya wananchi wanakwenda nje ya nchi kutibiwa moyo ambapo hadi sasa tumebakiza asilimia nne tu ya wagonjwa wa moyo wanaokwenda nje ya nchi kwa ajili ya kupatiwa matibabu ya moyo, asilimia hii nne tunaweza kuifuta kabisa kama wataalam wa CZRH mtajitoa kuifanya hospitali hii kuwa hospitali bingwa ya magonjwa ya moyo”, alisema Prof. Mahalu

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema kuwa JKCI imejipanga kuwafuata wananchi walipo ambapo kwa kuanza JKCI itaanzisha vituo viwili vya kuchunguza magonjwa ya moyo kwa lengo la kusogeza huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo kwa wananchi.

“Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato ni moja ya kitua cha uchunguzi na matibabu ya moyo ambapo leo hii tumezindua kliniki ya matibabu ya moyo lakini pia Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mtwara nayo itakua kituo kingine cha kuhudumia wagonjwa wa moyo”

“Tumekuwa tukifanya kambi maalum za matiabu (outreach) katika mkoa wa Dar es Salaam na kuwafanya wananchi wa mikoa mingine kusafiri kufuata huduma hizo, lakini sasa tumeona nimuhimu kuwafuata wananchi walipo ili pia tuweze kutoa mafuzo kwa wataalam wa afya tutakaowakuta sehemu tunazopeleka huduma hizi”

Aidha Dkt. Kisenge alisema kuwa Kituo cha uchunguzi na matibabu ya moyo cha Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Chato kitakapoimarika kitakua kikitoa huduma za upasuaji mkubwa wa moyo na kuwekeza mtambo wa Cathlab ambao utatumika kutoa huduma za upasuaji wa moyo wa tundu dogo.

“Tunakwenda kutengeneza mpango mkakati wa kuhakikisha katika miaka mitano huduma za upasuaji wa moyo na matibabu kwa kutumia mtambo wa Cathlab zinafanyika hapa Chato ikiwa ni njia ya kuwasaidia wananchi wa kanda ya ziwa na nchi za jirani”, alisema Dkt. Kisenge

Naye mwananchi wa Chato aliyepatiwa huduma wakati wa kambi hiyo Omary Maulid alisema kuwa hakuwahi kujua kama anamatatizo ya shinikizo la damu na kisukari kwani mara zote alizokua akienda hospitali na kumweleza daktari kuwa macho hayaoni vizuri hakupimwa shinikizo la damu wala sukari hivyo kujikuta anatibiwa vitu vingine.

“Nimefurahi kupata fursa hii ya kuja kuchunguza afya ya moyo wangu kwasababu nimekua nikiumwa siku nyingi, macho yangu hayaoni vizuri kumbe nina shinikizo la juu la damu ambalo sikuwahi kupimwa leo hii ndio nimejitambua”,

“Elimu ya afya hasa hii ya magonjwa yasiyoambukiza inatakiwa kutolewa zaidi sio tu kwa wananchi lakini pia na kwa wataalam wa afya waliopo katika vituo vya afya katika jamii zetu ili wananchi tuweze kupata tiba sahihi pale tunapoumwa”, alisema Omary

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari