JKCI yaja na kampeni ya kuhamasisha jamii kufanya mazoezi kujikinga na magonjwa ya moyo
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akipokea leo jijini Dar es Salaam maT- shirt mawili kati ya 100 kutoka kwa Meneja mkuu wa Kampuni ya Ulinzi ya K4S Security Kemmy David zitakazotumika wakati wa matembezi ya Km.5 kuhamasisha wananchi kufanya mazoezi ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo.
Meneja Uendeshaji wa Kampuni ya Ulinzi ya K4S Security Joseph Goliama akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge leo jijini Dar es Salaam baadhi ya maT-shirt kati ya 100 yaliyotolewa na Kampuni hiyo zitakazotumika wakati wa kampeni ya kuhamasisha wananchi kufanya mazoezi kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na viongozi kutoka Kampuni ya Ulinzi ya K4S Security walipotembelea ofisini kwake leo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kumkabidhi T-shirt 100 ambazo zitakazotumika wakati wa kampeni ya kuwahamashisha wananchi kufanya mazoezi kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo.
Picha na Khamis Mussa
********************************************************************************************************************************************************************************
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) inatarajia
kuanzisha matembezi ya kilomita tano kwa ajili ya kuhamasisha jamii kujikinga
na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo ambayo yamekuwa
yakiongezeka kwa kasi duniani.
Akizungumza wakati wa kupokea maT-shirt 100 zilizotolewa na Kampuni ya Ulinzi ya K4S
Security leo jijini Dar ers Salaam ambazo zitavaliwa katika matembezi hayo Mkurugenzi
Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge alisema wameamua kuanzisha matembezi hayo ili
kuihamasisha jamii kuona umuhimu wa kufanya mazoezi na kijikinga na magonjwa hayo.
Dkt. Kisenge aliishukuru kampuni hiyo kwa kuwa sehemu ya
kuhamashisha jamii kujikinga na magonjwa ya moyo na kusema kuwa JKCI ina wajibu
wa kuhakikisha jamii inajikinga na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya
moyo ambayo yamekuwa yakisababisha vifo vya watu wengi duniani.
“Katika kuhakikisha jamii inakuwa salama Taasisi yetu hivi
karibuni inatarajia kuanzisha matembezi ambayo yatatoa motisha kwa jamii
kufanya mazoezi kama njia mojawapo ya kujikinga na magonjwa hayo,”.
“Tunatarajia kufanya matembezi ya kilomita tano angalau mara
moja kwa mwezi, matembezi ambayo yatahamasisha wananchi wakiwemo wafanyakazi wetu
kufanya mazoezi kwani moja ya kinga ya magonjwa ya moyo ni pamoja na kufanya
mazoezi,”alisema Dkt.Kisenge.
Dkt. Kisenge aliongeza kuwa magonjwa ya moyo yanaweza kuzuilika kama jamii
itafuata mtindo bora wa maisha ikiwemo kufanya mazoezi, kutokutumia bidhaa za
tumbaku, kula mlo bora pamoja na kuacha kutumia vilevi ambavyo ni hatari kwa
afya ya moyo.
Kwa upande wake Meneja Mkuu wa Kampuni ya Ulinzi ya K4S
Security Kemmy David alisema kampuni hiyo imeona ni vizuri kurudisha kwa jamii
mafanikio wanayoyapata wakiwa na lengo la kusaidia jamii ili iweze kujikinga na
magonjwa ya moyo.
“Hii ni mara yetu ya pili kama kampuni ya K4S Security
kushirikiana na JKCI kuhakikisha jamii inayotuzunguka inafaidika na uwepo wetu
kwani bila wao sisi tusingeweza kupata mafanikio tuliyonayo,”alisema David.
Meneja huyo alisema siku ya uzinduzi wa matembezi hayo
wafanyakazi wa K4S Security watakuwa sehemu ya matembezi ili nao wajijengee
tabia ya kufanya mazoezi kujilinda na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa
ya moyo.
Matembezi hayo ambayo yana kauli mbiu ya “Fanya Mazoezi na JKCI, Linda Moyo Wako” yanayotarajiwa kuzinduliwa hivi karibuni yatahusisha wafanyakazi wa Taasisi hiyo pamoja na wadau wengine wa afya.
Comments
Post a Comment