Madaktari Afrika watoa msaada wa vifaa tiba vya bilioni moja
Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel akiwa katika
picha ya pamoja na madaktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao
kutoka Shirika la Madaktari Afrika la nchini Marekani alipowatembelea kabla ya
kuanza kwa kambi maalum ya siku tano ya matibabu ya umeme wa moyo leo jijini
Dar es Salaam.
Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel akimsikiliza
Daktari bingwa wa moyo na mfumo wa umeme wa moyo kutoka Shirika la Madaktari
Afrika lililopo nchini Marekani David Singh alipotembelea Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) leo kwaajili ya kuonana na madaktari hao kabla ya kuanza
kwa kambi maalum ya matibabu ya umeme wa moyo ya siku tano inayofanyika JKCI.
Na: JKCI
***********************************************************************************************************************
Shirika la Madaktari Afrika lililopo nchini Marekani limetoa
msaada wa vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi bilioni moja ambavyo vitatumika
katika kambi maalumu ya siku tano ya matibabu ya mfumo wa umeme wa moyo.
Kambi hiyo iliyoanza leo katika Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) imelenga kubadilishana uzoefu baina ya wataalam wa afya wa JKCI
na wenzao kutoka Shirika la Madaktari Afrika, kuwasaidia wagonjwa vifaa vya matibabu hayo na
kutoa huduma ya matibabu ya mfumo wa umeme wa moyo.
Akizungumza na madaktari wanaotoa matibabu katika kambi hiyo alipowatembela leo jijini Dar es Salaam Naibu
Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel aliwashukuru Madaktari Afrika kwa msaada
walioutoa na kusemaa magonjwa ya mfumo wa umeme wa moyo ni sehemu ngumu kwenye
masuala ya tiba ya moyo hivyo kuwapongeza madaktari hao kwa kuwa mstari wa
mbele kushirikiana na wataalam wa JKCI kuokoa maisha ya watanzania.
“Rais wetu alishawekeza mtambo wa kisasa wa kutibu umeme wa
moyo, upande wa suala la tiba tumejitahidi kupata wataalam wenye uwezo wa kutoa
huduma bora kuendana na teknolojia iliyopo, hatuna budi kushirikiana nanyi
kwani muda mrefu mmekuwa mkitoa matibabu haya”, alisema Dkt. Mollel.
Dkt. Mollel alisema mbali na kubadilishana uzoefu madaktari
hao wamekuja wakijua yakuwa kuna watanzania wenye matatizo ya umeme wa moyo
lakini hawana uwezo wa kumudu gharama za matibabu hivyo kuleta vifaa vya matibabu
kuwatibu wasiokuwa na uwezo wa kugharamia matibabu.
“Kupitia kambi hii wataalam wetu wataenda kubadilishana
uzoefu na kuendeleza teknolojia katika kutoa huduma za matibabu ya mfumo wa umeme
wa moyo na kuifanya Taasisi hii kutambulika katika nchi nyingi zilizotuzunguka
hivyo badala ya kuwapeleka wagonjwa wao barani Ulaya sasa wanasaini mikataba na
JKCI ili wagonjwa wao watibiwe hapa nchini kutokana na uwezo wetu kupanda hadi
kufikia asilima 97”, alisema Dkt. Mollel.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema madaktari kutoka Shirika la Madaktari
Afrika wamekuja na vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi bilioni moja ili
kuwasaidia wagonjwa wasiokuwa na uwezo wa kugharamia matibabu hayo.
“Madaktari Afrika ni marafiki zetu ambao wamekuwa wakishirikiana
nasi kwa muda mrefu, wamefika hapa kwaajili ya kuwafundisha madaktari wetu na
kuwasaidia wagonjwa wenye matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo kutokufanya kazi
vizuri”, alisema Dkt. Kisenge
Dkt. Kisenge alisema katika kambi hiyo wagonjwa wenye
matatizo makubwa ya mfumo wa umeme wa moyo watapatiwa matibabu na mabingwa hao
wakiwa na lengo la kutoa huduma za matibabu pamoja na kubadilishana uzoefu na
madaktari, wauguzi na wataalam wa kuendesha mtambo wa Cathlab.
Naye Daktari bingwa wa mfumo wa umeme wa moyo kutoka Shirika
la Madaktari Afrika David Singh alisema katika kambi hiyo wanashirikiana na
madaktari wa JKCI kujifunza mbinu mpya za matibabu ya mfumo wa umeme wa moyo ili
kuendana na maendeleo ya teknolojia ya matibabu.
“Tumefika katika Taasisi hii kwasababu tuna taarifa za huduma
bora zinazotolewa kwa wagonjwa wanaotibiwa hapa, hivyo tukaona ni sehemu sahihi
ambayo tunaweza kushirikiana na kuboresha huduma zaidi”, alisema Dkt. David.
Dkt. David alisema Shirika la Madaktari Afrika litaendelea
kushirikiana na wataalam wa Afya wa JKCI kwani kwa sasa Taasisi hiyo inafanya
vizuri katika utoaji wa uchunguzi na matibabu ya moyo Afrika Mashariki na kati.
Comments
Post a Comment