Wapigwa msasa wa kuwahudumia wagonjwa wa dharura na mahututi
Mkurugenzi wa Upasuaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya akitoa neno na shukrani wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku mbili ya kuwahudumia wagonjwa wa dharura na mahututi yanayotolewa kwa wafanyakazi wa Kurugenzi hiyo leo jijini Dar es Salaam.
Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Godwin Sharau akichangia mada wakati wa mafunzo ya siku mbili ya kuwahudumia wagonjwa wa dharura na mahututi yanayofanyika katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
**************************************************************************************************************************************************************************************************************************************
Wataalamu wa magonjwa ya moyo 100 kutoka Kurugenzi
ya Upasuaji ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wamepatiwa mafunzo ya
kuongeza ujuzi wa jinsi ya kuwahudumia wagonjwa wa dharura na mahututi.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge
aliipongeza Kurugenzi ya upasuaji kwa kuwa na wazo la kuikutanisha Kurugenzi
nzima kupata mafunzo hayo kwani ni ya muhimu katika kuokoa maisha ya wagonjwa
wengi wanaotibiwa katika Taasisi hiyo.
“Kumuhudumia mgonjwa aliye mahututi sio kazi ya mtu mmoja
inahitaji timu ya wataalamu wa afya mbalimbali walio na mafunzo ya kiwango cha
juu cha kuokoa maisha kama ambavyo Kurugenzi yenu imekuwa ikifanya na kuongeza ujuzi mara
kwa mara”, alisema Dkt. Kisenge.
Dkt. Kisenge alisema ni muhimu kwa mafunzo hayo ya siku mbili yakabadilishe muenendo wa kutoa huduma kwa wagonjwa wa
dharura na mahututi na kupokea mawazo kwa kila mshiriki kwani huduma ya dharura
inahitaji ushirikiano wa pamoja.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Upasuaji wa Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya alisema hii ni mara ya pili kurugenzi
hiyo kuandaa mafunzo hayo yanayohusisha mafunzo kwa vitendo ili kila mtaalamu
wa afya aweze kuona kwa uhalisia vifaa vinavyotumika na kufanya mazoezi kwa
vitendo.
“Wakati wa upasuaji mgonjwa anaweza akabadilika na kuhitaji
matibabu ya dharura hivyo kama wahusika wakuu wa huduma za upasuaji lazima kila
mfanyakazi ajue ni kitu gani kinatakiwa kufanyika ili kuokoa maisha ya
mgonjwa”, alisema Dkt. Angela.
Dkt. Angela alisema mafunzo hayo yameandaliwa kwa lengo la
kusaidia wataalamu wa Kurugenzi ya Upasuaji kuwa katika viwango vya kimataifa
vya kutoa huduma inayoendana na
maendeleo ya sayansi na teknolojia yaliyopo.
“Mafunzo ya kuwahudumia wagonjwa wa dharura na mahututi ni ya
muhimu kwetu sisi kwasababu tunaamini kama wataalam wa afya tunatakiwa tuweze
kuwa na utayari wa kuwahudumia wagonjwa wakati wowote”, alisema Dkt. Angela.
Washiriki wa mafunzo hayo ni wataalamu kutoka Hospitali
ya JKCI Dar Group, madaktari wa
upasuaji, wataalam wa kuendesha mashine mbadala wakati wa upasuaji, wauguzi
wanaofanya kazi katika chumba cha upasuaji na chumba cha wagonjwa wanaohitaji
uangalizi maalum (ICU) na wauguzi wanaojifunza kuwahudumia wagonjwa wa dharura.
Comments
Post a Comment