Safari ya Uhai: Ushirikiano wa JKCI na NMB waokoa maisha ya watoto

Mtoto aliyelazwa katika wodi ya watoto wenye magonjwa ya moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Ester Ezekiel akimkabidhi ua  Mtendaji Mkuu wa benki ya NMB Ruth Zaipuna alipotembelea Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kabla ya hafla fupi ya kuipongeza benki hiyo kwa mchango wanaoutoa katika matibabu ya moyo kwa watoto leo jijini Dar es Salaam. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimkabidhi zawadi Mtendaji Mkuu wa benki ya NMB Ruth Zaipuna wakati wa hafla fupi ya kuipongeza benki hiyo kwa mchango wanaoutoa katika matibabu ya moyo kwa watoto leo jijini Dar es Salaam. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge, na Mtendaji Mkuu wa benki ya NMB Ruth Zaipuna wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi JKCI baada ya kumalizika kwa hafla fupi ya kuipongeza benki hiyo kwa mchango wanaoutoa katika matibabu ya moyo kwa watoto leo jijini Dar es Salaam.

 


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge, na Afisa Mtendaji Mkuu wa benki ya NMB Ruth Zaipuna wakiwa pamoja na mmoja wa watoto wanaopatiwa matibabu ya moyo katikaTaasisi hiyo mara baada ya kumalizika kwa hafla fupi ya kuipongeza benki hiyo kwa mchango wanaoutoa katika matibabu ya moyo kwa watoto leo jijini Dar es Salaam.

Na JKCI
***************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kushirikiana na Benki ya NMB kuwafuata wanachini mahali walipo kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati wa hafla fupi ya kuipongeza benki hiyo kwa mchango wanaoutoka katika matibabu ya moyo kwa watoto wanaotibiwa JKCI.

Dkt. Kisenge ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo na mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo alisema NMB imedhamiria kufikisha elimu ya magonjwa ya moyo kupitia mikutano ya elimu ya fedha wanayofanya katika jamiii mbalimbali nchini.

"NMB inawajali wananchi, tunawashukuru sana kwa kuwa sehemu ya JKCI kuhakikisha jamii inayohitaji matibabu ya moyo inayapata kwa wakati", alisema Dkt. Kisenge.

Naye Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB Ruth Zaipuna alisema baada ya kuona uhitaji uliopo katika huduma za matibabu ya moyo benki hiyo iliona ni vyema kushiriki katika kuokoa maisha ya watoto na kurudisha furaha kwa wazazi wanaopitia changamoto za kuuguza.

“Kutokana na ukubwa wa matatizo haya ya moyo na jamii kubwa kushindwa kugharamia matibabu, wakati wa hafla ya chakula cha jioni iliyofanyika mwaka jana tuliahidi kuchangia shilingi bilioni 1 kwa kipindi cha miaka minne lakini leo tumetimiza mwaka mmoja tu na tumeshatoa nusu ya fedha tuliyoahidi”, alisema Ruth.

Ruth alisema NMB itaendelea kushirikiana na JKCI kwa karibu kuwasaidia watoto wanaohitaji upasuaji wa moyo kwani Taasisi hiyo ni tegemeo kwa watanzania na watu kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Shirika lisilo la Kiserikali la Heart Team Africa Foundation (HTAF) ambalo liliratibu chakula cha jioni cha kuchangisha fedha za matibabu ya moyo kwa watoto Dkt. Naizihijwa Majani alisema kwa kipindi cha mwaka mmoja NMB imeweza kuchangia shilingi milioni 500 katika matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa JKCI.

Dkt. Naizihijwa alisema     kupitia HTAF jumla ya watoto 185 wamefanyiwa upasuaji wa moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kipindi cha mwaka mmoja ambapo watoto 125 wametibiwa kupitia fedha zilizotolewa na NMB.

“NMB wamekuwa kinara katika kuchangia matibabu ya watoto, kupitia hafla ya chakula cha jioni iliyofanyika mwaka 2024 waliahidi shilingi billion 1 kwaajili ya matibabu ya watoto 250 ambapo hadi Leo wameshatoa fedha za matibabu ya watoto 125 na wote wameshapatiwa matibabu", alisema Dkt. Naizihijwa

Akitoa neno la shukrani mzazi ambaye mtoto wake ametibiwa na fedha zilizotolewa na NMB Veronica Temba aliishukuru JKCI na NMB kuwasaidia kupata huduma za matibabu ya moyo kwani gharama za matibabu hayo kwake zilikuwa kubwa hivyo familia yake isingeweza kuzimudu.

“Mwanangu amefanyiwa upasuaji, namshukuru Mungu anaendelea vizuri kwani gharama za matibabu zilikuwa kubwa hivyo sikuweza kuzimudu lakini kupitia NMB mwanangu ameweza kutibiwa”, alisema Veronica.

Veronica aliiomba NMB kuendelea kuwasaidia watoto wengine wanaohitaji matibabu ya moyo kwani watoto wengi wanatoka katika familia zisizokuwa na uwezo wa kugharamia matibabu hayo.

 

 

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na Burkina Faso zasaini makubaliano ya ushirikiano katika kutoa tiba ya magonjwa ya moyo

Wagonjwa wenye matatizo ya mishipa ya damu ya miguu kutanuka kutibiwa JKCI

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi