Wanamichezo 450 Wapimwa Afya ya Moyo Katika Mashindano ya Chipukizi Cup Arusha
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Eva Wakuganda akimpima kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi mchezaji aliyeshiriki mashindano ya 16 ya Chipukiz Cup yaliyomalizika hivi karibuni katika viwanja vya Tanganyika Game Trackers (TGT) vilivyopo jijini Arusha.
Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group, Mkurugenzi wa Future Stars Alfred Itaeli, Kocha wa timu za vijana kutoka Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Haruna Adolph na kamati ya mashindano mkoa wa Arusha wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa mashindano ya 16 ya Chipukizi Cup yaliyomalizika hivi karibuni katika viwanja vya Tanganyika Game Trackers (TGT) vilivyopo jijini Arusha.
*********************************************************************************************************************************************************************************************
Wanamichezo 450 kutoka mataifa mbalimbali barani Afrika walioshiriki mashindano ya 16 ya Chipukizi Cup yaliyofanyika jijini Arusha wamefanyiwa uchunguzi wa afya ya moyo, hatua inayolenga kuimarisha usalama na ustawi wa wanamichezo chipukizi.
Zoezi hilo lilifanyika hivi karibuni katika
viwanja vya Tanganyika Game Trackers (TGT), ambapo wataalamu wa moyo kutoka
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group waliwahudumia
wanamichezo hao kwa kufanya vipimo mbalimbali vya moyo.
Akizungumza wakati wa kuhitimisha zoezi hilo Daktari
bingwa wa bagonjwa ya moyo kwa watoto wa JKCI Hospitali ya Dar Group Eva Wakuganda alisema matokeo
ya awali yalionyesha hali nzuri ya afya ya moyo kwa wanamichezo wengi, hali
iliyowawezesha kuendelea na mazoezi pamoja na kushiriki mashindano bila
kikwazo.
Alisema wanamichezo hao walifanyiwa vipimo
muhimu ikiwemo kipimo cha kuchunguza mfumo wa umeme wa moyo (ECG) pamoja na
kipimo cha kutathmini muundo na utendaji wa moyo (ECHO), vipimo vinavyosaidia
kugundua mapema changamoto za kiafya.
“Vipimo vya awali
vilionesha kuwa wanamichezo wengi wako salama kiafya, hivyo tuliwaruhusu
kuendelea na michezo. Hata hivyo, wachache tulibaini kuwa na changamoto
zilizohitaji uchunguzi wa kina zaidi,” alisema Dkt. Eva.
Aliongeza kuwa baadhi ya wanamichezo
waliripoti dalili kama maumivu ya kifua na kizunguzungu wakati wa mazoezi hali
iliyowalazimu kufanyiwa vipimo zaidi na kushauriwa kufika JKCI kwa uchunguzi wa
kina ikiwemo kipimo cha Stress ECG.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Future Stars
Academy, Alfred Itaeli aliipongeza JKCI kwa mchango wake mkubwa katika kulinda
afya za wanamichezo, akisema huduma hiyo imewasaidia vijana kutambua mapema
hali zao za kiafya na kuzuia madhara makubwa ya baadaye.
“Hii ni fursa
muhimu kwa vijana kutambua afya zao mapema. Kuingiza huduma za Sports Medicine
kuanzia ngazi za chini ni hatua kubwa katika maendeleo ya michezo nchini,” alisema Itaeli.
Wanamichezo walioshiriki mashindano hayo nao
wameeleza kuridhishwa na huduma ya uchunguzi wa moyo, wakisema imewaongezea
uelewa kuhusu umuhimu wa afya katika taaluma ya michezo.
Mchezaji wa Dream Catchers Academy kutoka
Zimbabwe, Beloved Rusakaniko alisema kupima afya ya moyo kumempa uhakika wa
kuendelea na michezo kwa kujiamini zaidi.
“Nimefurahi sana
kupima moyo wangu na kupata majibu kuwa uko salama. Kwa wanamichezo, afya ya
moyo ni msingi wa mafanikio,”
alisema Rusakaniko.
Naye mchezaji wa Arusha Youth Development
Organization Academy, Aisha Ramadhan, alisema afya ndiyo mtaji mkubwa kwa
mchezaji yeyote.
“Ni mara yangu ya
kwanza kupima moyo na nimejifunza kuwa bila afya huwezi kufikia malengo yako
kama mchezaji,”
alisema Aisha.
Mashindano ya 16 ya Chipukizi Cup yalifanyika kwa siku saba kuanzia tarehe 15 hadi 21 Desemba 2025 katika viwanja vya Tanganyika Game Trackers (TGT) jijini Arusha.




Comments
Post a Comment