JKCI, MSD kuwafuata wananchi Arusha kupima magonjwa ya moyo

Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Janeth Mmari akimfafanulia mwananchi kuhusu magonjwa ya moyo mara baada ya kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo wakati wa kambi maalumu iliyofanywa na Taasisi hiyo kabla ya kuanza kwa mechi ya mpira wa miguu baina ya mashabiki wa timu za Simba na Yanga jana katika Uwanja wa mpira wa KMC uliopo Mwenge jijini Dar es Salaam.
******************************************************************************************************************************************************************************************************************
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa
kushirikiana na Bohari ya Dawa (MSD) itafanya kambi maalumu ya upimaji na matibabu
ya magonjwa mbalimbali yakiwemo ya moyo kwa
wananchi wa Mkoa wa Arusha na mikoa ya jirani kuanzia Desemba 29, 2025 hadi Januari 5,
2026, katika Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre
(ALMC).
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini
Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa
JKCI, Dkt. Peter Kisenge alisema taasisi hiyo imefanya upimaji wa
magonjwa ya moyo katika mikoa zaidi ya
16, ambapo wagonjwa zaidi ya 23,000
walihudumiwa, huku mikoa ya Kanda ya Kaskazini ikionesha uhitaji mkubwa zaidi
wa huduma hizo.
“Tunaenda kufanya
upimaji na kutoa elimu ya afya ya moyo ili kuokoa wananchi wengi wasiendelee
kupata madhara yatokanayo na magonjwa haya,” alisema Dkt. Kisenge.
Alisema kambi hiyo itahusisha upimaji wa magonjwa mbalimbali yakiwemo ya moyo na magonjwa yasiyoambukiza, kwa
watoto na watu wazima, na huduma zitatolewa kuanzia saa 2:00 asubuhi hadi saa 10:00 jioni.
Dkt. Kisenge aliongeza kuwa Hospitali ya
Arusha Lutheran Medical Centre imeingia ushirikiano
wa miaka 20 na JKCI, ambapo kuanzia Januari 1, 2026, hospitali hiyo itasimamiwa na JKCI kwa lengo la
kusogeza huduma bora za moyo na matibabu ya magonjwa mengine karibu na wananchi
wa Kanda ya Kaskazini.
“Tunaendelea
kuonesha utu kwa kuwafuata wananchi walipo ili kuokoa maisha yao. Tunawasihi
wananchi kuhakikisha wanazingatia afya ya mioyo yao na kubadili mitindo ya
maisha,” alisisitiza.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Matibabu ya Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Dkt. Tatizo Waane, alisema zaidi ya asilimia 25 ya wagonjwa wanaopata huduma JKCI wanatoka Kanda ya Kaskazini,
hivyo ushirikiano huo utasaidia kwa kiasi kikubwa kusogeza huduma karibu na
wananchi.
“Uwepo wetu Arusha
utapunguza gharama za kufuata huduma mbali, kuboresha huduma za moyo na
kujiandaa kwa ongezeko la watalii wanaotembelea mbuga za wanyama, Mlima
Kilimanjaro pamoja na maandalizi ya mashindano ya AFCON,” alisema Dkt. Waane ambaye pia ni
baktari bingwa wa moyo na mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba.
Naye Meneja
Mawasiliano na Uhusiano wa Bohari ya Dawa (MSD), Etty Kusiluka, alisema
katika kambi hiyo MSD itahakikisha upatikanaji
wa dawa na vifaa tiba kwa wakati kupitia Kanda ya Kaskazini ya MSD iliyopo Kilimanjaro, ili kuhakikisha
huduma za matibabu zinatolewa kikamilifu.
“Wakati JKCI
inasogeza huduma kwa wananchi, sisi tutahakikisha vifaa na dawa muhimu
vinapatikana ili kukamilisha matibabu yote yanayohitajika. Tuko tayari kwa
ushirikiano huu,”
alisema Etty.
Comments
Post a Comment