Stanbic Benki yaokoa maisha: Yaipatia JKCI vifaa tiba vya moyo vya milioni 20


Mkurugenzi wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane akipokea msaada wa vifaa tiba venye thamani ya shilingi milioni 20 kutoka kwa Meneja Mwandamizi Matawi ya Stanbic Benki Tanzania Edditrice Marco vilivyotolewa na benki hiyo hivi karibuni ambavyo vitatumika kwa wagonjwa wanaotibiwa katika taasisi hiyo.


 Mkurugenzi wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane akitoa neno la shukrani a mara baada ya kupokea vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 20 kutoka Benki ya Stanbic kwaajili ya wagonjwa wanaotiwa katika taasisi hiyo.

************************************************************************************************************************************************************************************

Benki ya Stanbic Tanzania imekabidhi msaada wa vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 20 kwa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) hatua inayolenga kuimarisha huduma za matibabu kwa wagonjwa wa moyo wanaohitaji uangalizi maalumu.

Msaada huo uliotolewa hivi karibuni unajumuisha mashine tatu za cardiac monitor zenye thamani ya shilingi milioni 18 pamoja na mashine moja ya syringe pump yenye thamani ya shilingi milioni 2, ambazo zitatumika katika wodi ya uangalizi maalumu (HDU) kwa wagonjwa wa moyo wanaolazwa katika taasisi hiyo.

Akizungumza wakati wa hafla ya kupokea vifaa hivyo, Mkurugenzi wa Magonjwa ya Moyo wa JKCI,  Dkt. Tatizo Waane aliushukuru uongozi wa Benki ya Stanbic kwa msaada huo, akisema ni mchango muhimu katika kuboresha huduma kwa wagonjwa wanaohitaji ufuatiliaji wa karibu wa hali zao za kiafya.

Dkt. Waane alisema kwa sasa JKCI inawahudumia wagonjwa wengi wenye hali tofauti za kiuchumi, hivyo upatikanaji wa mashine hizo utasaidia kupunguza changamoto kwa wagonjwa wanaohitaji huduma za cardiac monitor lakini hawana uwezo wa kugharamia gharama za matibabu.

“Vifaa hivi vitasaidia kuokoa maisha ya wagonjwa wengi, hasa wale wanaohitaji uangalizi wa saa 24. Ni msaada unaogusa moja kwa moja mahitaji halisi ya wagonjwa wetu,” alisema Dkt. Waane ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo na mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba.

Kwa upande wake Meneja Mwandamizi wa Matawi wa Benki ya Stanbic Tanzania, Edditrice Marco alisema benki hiyo imeamua kutoa msaada huo kama sehemu ya kutimiza wajibu wake wa kuchangia maendeleo ya jamii inayowazunguka hususan katika sekta nyeti ya afya.

Edditrice alisema wafanyakazi wa Benki ya Stanbic wameungana na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete katika kuunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuboresha utoaji wa huduma za afya nchini, kwa kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na za kisasa.

Aliongeza kuwa Benki ya Stanbic inaamini kuwa utoaji wa huduma bora kwa jamii huanza na moyo wa kujitolea, akisisitiza kuwa huo ndio msingi wa falsafa ya benki hiyo katika kutekeleza miradi ya uwajibikaji kwa jamii (CSR).


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na Burkina Faso zasaini makubaliano ya ushirikiano katika kutoa tiba ya magonjwa ya moyo

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi

Msumbiji kushirikiana na JKCI katika tiba ya moyo