Safari za matibabu zapungua: Kambi maalumu ALMC yawanufaisha wagonjwa wa mishipa ya damu na figo
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Salehe Mwinchete akimuhudumia mwananchi wa Arusha aliyefika kufanyiwa uchunguzi na matibabu ya moyo katika kambi maalumu ya upimaji na matibabu ya magonjwa mbalimbali yakiwemo ya moyo inayofanyika Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) iliyopo jijini Arusha.
Daktari wa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Winnie Masakuya akimpima mtoto kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi katika kambi maalumu ya siku nane ya upimaji na matibabu ya magonjwa mbalimbali yakiwemo ya moyo inayofanyika Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC).
Wakazi wa jiji la Arusha wakisubiri kupata huduma ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali zinazotolewa katika kambi maalumu ya matibabu yakiwemo ya moyo inayofanyika Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC).
****************************************************************************************************************************************************************************************************
Wagonjwa wanaosumbuliwa na matatizo ya mishipa ya damu kutanuka miguuni pamoja na wanaohitaji kuwekewa njia za kusafisha damu wameombwa kujitokeza katika kambi maalumu ya matibabu ya magonjwa mbalimbali inayoendelea katika Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Center (ALMC) ili kupata huduma za kibingwa kwa karibu.
Wito huo umetolewa leo na Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo na Mishipa
ya Damu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete, Alex Joseph wakati
akizungumza na waandishi wa habari kuhusu huduma zinazotolewa katika kambi
hiyo.
Dkt. Alex alisema wagonjwa wenye matatizo ya
figo wanapatiwa huduma ya kuwekewa njia za kusafisha damu, kitaalamu
zikijulikana kama fistula na permanent catheter huduma ambazo mara
nyingi hupatikana katika hospitali chache za rufaa.
“Katika kambi hii tunatoa pia huduma za
uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya upasuaji wa mishipa ya damu, moyo na
kifua. Tunawahimiza wananchi wenye matatizo ya mishipa ya damu isiyopitisha
damu vizuri kufika ALMC ili waweze kuhudumiwa,” alisema Dkt. Alex.
Aliongeza kuwa tangu kuanza kwa kambi hiyo, wametoa
huduma kwa wagonjwa 25 wenye
matatizo ya mishipa ya damu pamoja na wanaohitaji kuwekewa njia za kusafisha
damu, ambapo wagonjwa saba tayari
wamefanyiwa upasuaji na hali zao zinaendelea vizuri huku wengine
wakiruhusiwa kurejea nyumbani.
Kwa upande wao wagonjwa waliopata huduma
katika kambi hiyo walishukuru juhudi za wataalamu wa afya, wakisema huduma hizo
zimewapunguzia gharama na usumbufu wa kusafiri umbali mrefu kufuata matibabu.
“Nimefurahi sana kupata huduma ya kuwekewa
njia ya kusafisha damu hapa ALMC. Nimewekewa permanent catheter jana na leo nimeruhusiwa. Nawahamasisha
wagonjwa wengine wenye uhitaji huu kufika hapa,” alisema Elifuraha Mbise mkazi wa Ngaramtoni.
“Mtoto wangu amefanyiwa vipimo vya moyo na
damu bila gharama. Nawaomba wazazi wenye watoto wenye matatizo mbalimbali
wafike ALMC kwani huduma zinapatikana,” alisema.
Naye Simon
Kivuyo mkazi wa Kiseriani, aliwashukuru wataalamu wa afya kwa huduma
alizopata na kusema kuwa wamepima vipimo mbalimbali vikiwemo vya moyo. Aliwahimiza
wananchi watumie fursa hiy kupima afya zao mapema.
Kwa muda wa siku mbili tangu kuanza kwa kambi hiyo wananchi 312 wamejitokeza kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali, yakiwemo ya moyo kwa watoto na watu wazima.
Comments
Post a Comment