Watu 1,089 wamefanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo kambi maalumu ya Mhe. Makonda
Wananchi kutoka mikoa
mbalimbali ya Kaskazini wakiwa katika foleni ya kupata huduma za uchunguzi na
matibabu ya magonjwa ya moyo wakati wa kambi maalumu ya kupima na kutibu
magonjwa ya binadamu iliyoandaliwa na Ofisi ya Mbunge wa Arusha mjini Mhe. Paul
Makonda na kufanyika katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha. Jumla ya
watu 1,089 wamepimwa moyo.
Daktari wa Hospitali ya
Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) ambayo inasimamiwa na Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) Adda Justine akimpatia maelekezo mwananchi aliyefika
kufanya uchunguzi wa afya wakati wa kambi maalumu ya kupima na kutibu magonjwa
ya binadamu iliyoandaliwa na Ofisi ya Mbunge wa Arusha mjini Mhe. Paul Makonda
na kufanyika katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha. Jumla ya watu
1,089 wamepimwa moyo.
Mbunge wa jimbo la
Arusha mjini Mhe. Paul Makonda akizungumza na wananchi waliokuwa wakisubiri
kupata huduma katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa
kambi maalumu ya kupima na kutibu magonjwa ya binadamu iliyokuwa ikifanyika
katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid na kumalizika leo jijini Arusha. Jumla ya
watu 1,089 wamepimwa moyo.
Na JKCI
***************************************************************************************************
Watu 1,089 wakiwemo
wanawake 818 na wanaume 271 wamefanyiwa uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya
moyo katika kambi maalumu ya uchunguzi wa magonjwa ya binadamu iliyomalizika
leo jijini Arusha.
Kambi hiyo
iliyoandaliwa na Mbunge wa jimbo la Arusha mjini Mhe. Paul Makonda
imeshirikisha hospitali zinazotoa huduma bingwa bobezi nchini ambapo watu zaidi
ya elfu 13 wamefanyiwa uchunguzi wa magonjwa mbalimbali ya binadamu.
Akizungumza wakati wa
kufunga kambi hiyo daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) Salehe
Mwinchete alisema watu 739 walifanyiwa uchunguzi kwa kupimwa kipimo cha
kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography - ECHO).
“Kupitia kambi hii
tumeweza kuwafanyia watu 777 kipimo cha kuangalia mfumo wa umeme wa moyo
(Electrocardiography - ECG) ambapo baadhi yao waligundulika kuwa na matatizo ya
mfumo wa umeme wa moyo na kuwapa rufaa kwaajili ya uchunguzi zaidi”, alisema
Dkt. Salehe
Dkt. Salehe alisema
katika kambi hiyo pia kulikuwa na daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto
ambaye alitoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo kwa watoto 63 waliohitaji
huduma za moyo.
“Tumetoa rufaa kwa watu
119 kwenda katika matawi yetu kwaajili ya uchunguzi zaidi, watu hawa tumewakuta
na matatizo mbalimbali ya moyo ikiwemo magonjwa ya shinikizo la damu, sukari
kwenye damu, matatizo ya hitilafu ya mfumo wa umeme wa moyo, moyo kutanuka,
matatizo ya kuziba kwa mishipa ya damu ya moyo, moyo kushindwa kufanya kazi na
matundu ya moyo kwa watoto”, alisema Dkt. Salehe
Kwa upande wa wananchi
waliopata huduma katika banda la JKCI wakati wa kambi hiyo wamewapongeza
wataalamu wa JKCI kwa kutoa huduma kwa upendo bila kuchoka na kuhakikisha watu
wote waliohitaji huduma za moyo wanazipata.
Daud Olesekei alisema huduma
aliyoipata katika banda la JKCI imemsaidia kujitambua, kuchukua hatua za mapema
na kufuata ushauri wa wataalamu wa afya ile magonjwa ya moyo aliyonayo
yasimdhuru zaidi.
“Nimefurahi sana kupata
huduma katika banda la JKCI, tunamuomba Mhe. Makonda aendelee kutuletea
wataalamu hawa ili hata sisi tusiokuwa na uwezo wa kuzifuata huduma bingwa za
uchunguzi wa magonjwa ya moyo mahali zilipo tuweze kuzipata”, alisema Daud.
Naye Catherine Tarimo
mkazi wa Kilimanjaro aliiomba Serikali iangalie namna ya kufanya kambi kama
hiyo katika mikoa yote ya Tanzania kuwasaidia wananchi wake kupata huduma za
afya na dawa pale inapohitajika.
“Nimetoka Kilimanjaro
hadi hapa Arusha kwaajili ya kambi hii ya Mhe. Makonda, nimefurahi nimepata
huduma na baada ya huduma nimepata dawa bila gharama yotote”, alisema
Catherine.
Kambi maalumu ya
uchunguzi wa magonjwa ya binadamu mkoani Arusha inayoratibiwa na Ofisi ya
Mbunge wa jimbo la Arusha mjini Mhe. Paul Makonda imefanyika kwa siku saba na
kuhudumia wananchi kutoka mkoa wa Arusha na mikoa ya jirani.



Comments
Post a Comment