Wananchi wapongeza huduma zinazotolewa na JKCI Maonesho ya Sabasaba
Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Emmanuel Lingido akimfundisha aina na makundi ya vyakula mwananchi aliyetembela banda la Taasisi hiyo wakati wa maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.
Afisa
Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Idd Kimario akimpima joto la
mwili mwananchi aliyetembelea banda la Taasisi hiyo wakati wa maonesho ya 50 ya
Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayofanyika katika viwanja
vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa jijini Dar es
Salaam.
Na JKCI
******************************************************************************************************
Wananchi
wanaotembelea Kliniki ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo katika
Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) wamepongeza
huduma za uchunguzi wa afya, elimu na ushauri wa kitaalamu zinazotolewa na
wataalamu wa taasisi hiyo.
Wamesema
huduma hizo zinawasaidia kutambua mapema hali zao za afya na kupunguza hatari
ya magonjwa yasiyoambukiza hususan magonjwa ya moyo pamoja na kuwajengea uelewa
wa namna ya kuishi maisha yenye afya ili kujikinga na magonjwa hayo.
Mwanasheria
kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Muhidin Mapeyo alisema ameridhishwa na hatua ya
JKCI kusogeza huduma hizo muhimu za afya karibu na wananchi kupitia maonesho
hayo.
“Nimepata
fursa ya kutembelea banda la JKCI kwa sababu linatoa huduma muhimu
zinazowawezesha wananchi kufahamu hali zao za afya. Nimepokelewa vizuri, na
kabla ya kufanyiwa vipimo nilipatiwa maelezo yaliyonifanya nijisikie huru na
tayari kupata huduma”, alisema Mapeyo.
Aliongeza
kuwa mbali na vipimo vya afya wananchi pia wanapatiwa elimu kuhusu magonjwa
yasiyoambukiza na namna ya kubadili mtindo wa maisha ili kupunguza hatari ya
kupata magonjwa hayo.
Kwa
upande wake mkazi wa Kilimanjaro Barakaeli Mrema alisema ametembelea banda la
JKCI na kunufaika na elimu ya lishe bora pamoja na ushauri wa kitaalamu ambao
hakuwahi kuupata hapo awali.
“Kilichonifurahisha
zaidi ni ushauri wa lishe nilioupata, nimejifunza mbadala wa ulaji unaoweza
kunisaidia kuboresha afya yangu na kupunguza utegemezi wa dawa”, alisema Mrema.
Naye
mkazi wa Buza jijini Dar es Salaam Habiba Ally alisema ametumia fursa ya
maonesho hayo kupima afya yake na kupata ushauri kutoka kwa wataalamu bingwa wa
magonjwa ya moyo.
“Nimepima
uzito, urefu na kupata ushauri kutoka kwa wataalamu hawa wa moyo, pia
nimeshauriwa kupunguza uzito ili uendane na urefu wangu jambo ambalo litasaidia
kuboresha afya yangu”, alisema Habiba.
JKCI
inaendelea kutoa huduma za uchunguzi wa afya, elimu na ushauri wa kitaalamu
katika kliniki yake iliyopo Sabasaba ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhamasisha
jamii kutambua mapema hali zao za afya na kuchukua hatua za kujikinga na
magonjwa yasiyoambukiza.



Comments
Post a Comment