Benki ya NBC kuchangia kiasi cha shilingi bilioni 1 matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu
Nchemba akimkabidhi mfano wa hundi ya shilingi milioni 200 Mkurugenzi wa Tiba
Shirikishi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Naizihijwa
Majani kwaajili ya kuchangia matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo
wanaotibiwa JKCI iliyotolewa na Benki ya NBC kupitia mbio za NBC zilizofanyika
jana jijini Dodoma.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu
Nchemba akisalimiana na Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Dkt. Naizihijwa wakati wa mbio za NBC zilizofanyika jana katika
uwanja wa michezo Jamhuri uliopo jijini Dodoma.
Mjumbe wa bodi ya wadhamini wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) Dkt. Kassim Hussein akishiriki katika mazoezi ya viungo wakati wa mbio
za NBC zilizofanyika jana katika uwanja wa michezo Jamhuri uliopo jijini Dodoma
kwaajili ya kuchangia matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa
JKCI.
Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakionesha
medali zao mara baada ya kushiriki katika mbio za NBC zilizofanyika jana katika
uwanja wa michezo wa Jamhuri uliopo jijini Dodoma kwaajili ya kuchangia
matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa JKCI.
Benki ya NBC kuchangia shilingi bilioni 1 kwaajili ya
matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI).
Fedha hizo zinatarajiwa kutolewa kwa kipindi cha miaka mitano
mfululizo kupitia mbio za NBC ambapo mwaka huu zimefanyika jana jijini Dodoma
na kuchangia shilingi milioni 200 kwaajili ya matibabu ya watoto hao.
Akizungumza wakati wa mbio hizo jana jijini Dodoma Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mwigulu Nchemba alisema matumizi
ya fedha zilizotolewa kusaidia matibabu yaendane na thamani ya fedha hizo huku
yakitumika kwa uwazi ili malengo yaliyokusudiwa yaweze kuonekana.
“Ni muhimu kuona thamani ya kila senti inayotolewa na wadau
hawa kwa kuhakikisha fedha hizo zinatumika kwa kusudi lililokusudiwa na
kuwafikia walengwa wanaohitaji huduma za matibabu” alisema Mhe. Nchemba.
Mhe. Mwigulu alisema Serikali ya awamu ya sita itaendelea
kuwekeza katika Sekta ya Afya na kuhakikisha kuwa wadau wanaounga mkono
jitihada za serikali wanasaidiwa kwani kusudi la wadau na Serikali ni
kuhakikisha kuwa uhai wa watanzania unathaminiwa na kulindwa.
Aidha Mhe. Mwigulu aliwataka watanzania kuendelea kufanya
mazoezi kwaajili ya afya zao kwani afya bora ndio inayojenga taifa lenye uchumi
imara.
Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Benki ya NBC Theobald Sabi
alisema benki hiyo imeendelea kutekeleza wajibu wake kwa jamii kwa kuwekeza katika
sekta ya afya, elimu na maendeleo ya jamii, ambapo mwaka huu imetoa kiasi cha
shilingi milioni 200 kwa JKCI kama sehemu ya kurudisha kwa jamii na kuleta
furaha kwa watoto wenye magonjwa ya moyo.
“Tunatambua kuwa gharama za matibabu ya moyo ni kubwa hivyo
mchango huu umelenga kuwasaidia watoto wengi kupata huduma za matibabu kwa
wakati na kurejesha matumaini kwa familia zao. NBC itaendelea kuwa mshirika wa
maendeleo katika sekta ya afya kwa manufaa ya jamii”, alisema Sabi.
Sabi aliongeza kuwa mbio za NBC zimeendelea kuwa jukwaa
muhimu la kuunganisha wadau mbalimbali katika kusaidia jamii huku zikihamasisha
wananchi kufanya mazoezi na kuchangia katika huduma za afya.
Comments
Post a Comment