JKCI kuzifikia hospitali 15; kuwatafuta watoto wenye matatizo ya moyo

 

Madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa shirika la Little Heart la nchini Saudi Arabia ambalo ni moja ya mradi wa Afya ulioko ndani ya Taasisi ya Msaada ya Muntada yenye makao yake makuu jijini London nchini Uingereza wakimfanyia upasuaji wa kurekebisha mishipa ya damu mtoto ambaye mishipa yake ya damu ilikuwa inarudisha damu safi kutoka kwenye mapafu kwenda kwenye moyo upande wa kulia badala ya kupeleka damu hiyo upande wa kushoto wa moyo wakati wa kambi maalum ya ya upasuaji wa moyokwa watoto inayofanyika JKCI.

Picha na Khamisi Mussa

**************************************************************************************************************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imejipanga kuzifikia hospitali 15 zilizopo pembezoni mwa nchi kwa ajili ya kufanya uchunguzi na matibabu kwa  watoto wenye matatizo ya moyo ambao wakati mwingine wanaweza kupoteza maisha kutokana na kukosa huduma sahihi na kwa wakati.

Hayo yamesemwa hivi karibuni na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Dkt. Peter Kisenge wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu  kambi maalum ya upasuaji wa  moyo kwa watoto inayofanyika JKCI.

Dkt.Kisenge alisema watoto wenye matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo; matundu na mishipa ya damu ya moyo kutokukaa katika mpangilio wake kama wataweza kugundulika mapema na kupata huduma sahihi na kwa wakati wanapona na kuendelea na maisha kama watoto wengine.

“Tumejipanga kuendelea kutoa huduma za kibingwa kwa kuwafuata wananchi mahali walipo kwa kufanya hivyo tunawagundua wagonjwa wengi wenye matatizo ya  moyo ambao baada ya kuwafanyia upimaji tunawapa rufaa ya kuja kutibiwa JKCI na hivyo kupata  huduma za matibabu kwa wakati”, alisema Dkt. Kisenge.

Kuhusu  kambi hiyo ya ya upasuaji wa moyo kwa watoto alisema inayofanywa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao kutoka shirika la Little Heart la nchini Saudi Arabia ambao ni moja ya mradi wa Afya ulioko ndani ya Taasisi ya Msaada ya Muntada yenye makao yake makuu jijini London nchini Uingereza.

“Wenzetu hawa kutoka shirika la Little Heart walipofika kwetu mwaka 2015 wakati ambao uwezo wetu wa kutibu magonjwa ya moyo kwa watoto ulikuwa bado uko chini lakini wao waliweza kutusaidia kututoa pale tulipokuwa hadi sasa tunaweza kufanya upasuaji wa moyo wa aina mbalimbali kwa watoto wetu,”.

“Tutaendeleza mashirikiano haya ili taasisi yetu iendelee kuwa taasisi bora Afrika Mashariki na Kusini mwa jangwa la Sahara lakini pia tutahakikisha madaktari wetu wanapata ujuzi wa kutosha, tukiwa na lengo la kutoa huduma bora kwa watoto wetu wanaosumbuliwa na magonjwa ya moyo,” alisema Dkt. Kisenge.

Kwa upande wake daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Naiz Majani alisema shirika la Little Heart ambalo linatoa misaada kwa ajili ya upasuaji wa moyo kwa watoto lilikuwa kundi la kwanza la madaktari bingwa wa moyo kutoka nje ya nchi kwenda kufanya kambi za matibabu ya moyo kwa watoto wakati taasisi hiyo inaanzishwa.

Dkt. Naiz ambaye pia ni Mkuu wa kitengo cha kudhibiti na kuhakiki ubora wa huduma alisema Shirika hilo limekuwa likifanya upasuaji wa moyo kwa watoto wengi kwa kipindi cha wiki moja jambo ambalo limekuwa ni la tofauti ukilinganisha na upasuaji wa moyo unaofanywa na wataalam wengine.

 “Shirika la Little Heart lilipokuja kwa mara ya kwanza mwaka 2015 liliwashangaza watu kwani kwa kipindi cha siku saba waliweza kuwafanyia upasuaji wa moyo watoto 64. Hii ni mara yao ya sita toka walipoanza kuja hapa na wamekuwa wakiendelea kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto kwa idadi kubwa kwa kipindi kifupi kwa miaka yote ambayo wamekuwa wakitutembelea,”.

“Mpaka sasa wataalamu wa Shirika la Little Heart wameweza kufanya upasuaji wa moyo kwa kushirikiana na madaktari wa JKCI kwa watoto 352. Ujio wa mabingwa hawa kwa mara ya kwanza walikuja wataalam 32 lakini ujio wao wa sasa wamekuja wataalam 12 hii inaonyesha kuwa uwezo wa ndani wa JKCI umeongezeka”,alisema Dkt. Naiz.

Naye Meneja kutoka Shirika la Little Heart Kabir Miah alisema shirika hilo  linatoa huduma za upasuaji wa moyo kwa watoto wenye magonjwa ya moyo katika nchi mbalimbali zikiwemo nchi zilizopo kusini mwa jangwa la Sahara na Afrika.

 “Hii ni mara yetu ya sita kufika katika Taasisi hii kwa ajili ya kushirikiana na wataalam wa JKCI kutoa huduma za upasuaji wa moyo kwa watoto, kambi yetu ya kwanza ya mwaka 2015 tuliwafanyia upasuaji watoto 64, kambi ya pili mwaka 2016 tuliwafanyia upasuaji watoto 73”,.

“Kambi ya tatu mwaka 2017 tuliwafanyia upasuaji watoto 50, mwaka huo huo 2017 tulikuja mara ya pili Desemba na kuwafanyia upasuaji watoto 92, kambi ya tano ya mwaka 2018 tuliwafanyia upasuaji wa moyo watoto 73, na sasa kambi yetu ya sita tunatarajia kuwafanyia upasuaji wa moyo watoto 70”,.

“Tokea ujio wetu wa kwanza hapa JKCI hadi sasa tumeona mafanikio makubwa kwa wataalam waliopo hapa kwani mwaka 2015 upasuaji wa moyo kupitia tundu dogo kwenye paja kwa watoto ulikuwa haufanyiki lakini sasa hivi wataalam hawa wanafanya upasuaji huo,” alisema Kabir.

Kabir alisema wataalam kutoka shirika la  Little Heart wataendelea kushirikiana na JKCI katika kutoa huduma za matibabu ya moyo kwa watoto ikiwa ni sehemu ya msaada kama ambavyo mradi wa Afya ulioko ndani ya Taasisi ya Msaada ya Muntada unavyolenga kuwasaidi watoto wanaosumbuliwa na magonjwa ya moyo na kuwarejeshea matumaini ya kuishi.

Wataalamu walioko katika kambi hiyo walianza kufanya upasuaji tarehe 09/10/2020 na watamaliza  tarehe 14/10/2022 ambapo pamoja na kutoa huduma kwa wagonjwa pia kuna mafunzo mbalimbali yanayofanyika ikiwa ni pamoja na kubadilishana ujuzi wa kazi.


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)