Watu 1233 wafanyiwa upimaji na matibabu ya magonjwa ya moyo mkoani Arusha

Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao wa Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) wakiwa katika picha ya pamoja jana mara baada ya kumalizika kwa kambi maalum ya siku tano ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo kwa wakazi wa mkoa wa Arusha na mikoa jirani. Jumla ya watu 1233 wakiwemo watoto na watu wazima walifanyiwa uchunguzi katika kambi hiyo iliyoanza tarehe 26 hadi 30/09/2022.

**************************************************************************************************************************************************************************************

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Jumla ya watu 1233 wamefanyiwa upimaji na matibabu ya moyo katika kambi maalum ya matibabu iliyofanywa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC).

Kambi hiyo ya matibabu ya moyo iliyofanyika kwa siku tano ilianza tarehe 26 hadi 30/09/2022 ambapo watu wazima pamoja na  watoto walipata matibabu. Kambi hii  ilikuwa ni maalum kwa ajili ya  kuadhimisha siku ya moyo duniani iliyofanyika tarehe 29/09/2022.

Kwa upande wa watu wazima waliofanyiwa upimaji wengi wao walikutwa na matatizo ya shinikizo la juu la damu, kutanuka kwa moyo, kuziba kwa mishipa ya damu ya moyo na shida za valvu za moyo.

Watoto 70 walifanyiwa uchunguzi ambapo wengine walikutwa na matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo ambayo ni matundu na mishipa ya damu ya moyo kutokukaa katika mpangilio wake pamoja na valvu za moyo kuwa na shida.

Wagonjwa wengine kwa mara ya kwanza wamegundulika kuwa na matatizo ya moyo ikiwa ni pamoja na kutanuka na kuziba kwa mishipa ya damu ya moyo ambapo asilimia 5 tumewapa rufaa ya kuja kufanyiwa vipimo zaidi na kutibiwa katika Taasisi yetu.

Kwa upande wa watoto wenye matatizo tumewaelekeza kuja JKCI ili waweze kufanyiwa upasuaji katika kambi maalum za upasuaji wa moyo kwa watoto zitakazoanza tarehe 10/10/2022 na wengine watahudhuria kliniki zetu kwa ajili ya matibabu  na kuwafuatilia kwa ukaribu zaidi.

Katika kambi hii wananchi walipimwa vipimo mbalimbali vya moyo ikiwa ni pamoja na urefu, uzito, kiwango cha sukari mwilini, kuangalia uwiano baina ya urefu na uzito, kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography), mfumo wa umeme wa moyo (Electrocardiography) pamoja na vipimo vya damu (utendaji kazi wa figo, ini na kiwango cha mafuta kwenye damu).

Tulikuwa na wataalamu wa lishe ambao walitoa elimu ya lishe bora ambayo iliwapa wananchi kuwa na uelewa wa  kufuata mtindo bora wa maisha ambao utawasaidia kuepukana na magonjwa ya moyo ambayo ni moja ya magonjwa yasiyoambukiza na mtu anaweza kuyaepuka kwa kufuata ushauri wa kitaalamu.

Wananchi waliopata huduma za matibabu walitoka katika mikoa ya Arusha, Shinyanga, Singida, Mara, Kagera, Morogoro, Tanga, Manyara, Kilimanjaro na Iringa. Tumeona kuna uhitaji mkubwa wa huduma za kibingwa za matibabu ya moyo hiyo basi Taasisi yetu itaendelea kuwasogezea wananchi huduma hizi kwa kuwafuata mahali walipo.

Pia tutawajengea uwezo wataalamu wa afya wa jinsi ya kutambua na kutibu magonjwa ya moyo kwani Serikali imenunua mashine za kisasa za kuchunguza moyo na kuzisambaza katika Hospitali mbalimbali hapa nchini.

Tunawaomba wananchi muepuke tabia hatarishi zinazoweza kuharibu mioyo yenu hii ikiwa ni pamoja na uvutaji wa sigara na unywaji wa pombe uliokithiri. Zingatieni  mtindo bora wa maisha kwa kufanya mazoezi na kula vyakula bora.

“Tunajali Afya ya Moyo Wako”.

Imetolewa na :

Anna Nkinda

Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)