JKCI kuanzisha mpango wa wananchi wote kufanya mazoezi ya kutembea na kukimbia na ili kupunguza magonjwa ya moyo nchini
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Dkt. Peter Kisenge akipokea taarifa ya makabidhiano ya ofisi kutoka kwa
aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI ambaye sasa ni Mkurugenzi Mtendaji wa
Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) Prof. Mohamed janabi wakati wa makabidhiano
ya ofisi yaliyofanyika leo katika Taasisi hiyo Jijini Dar es Salaam
Mwenyekiti wa SACCOS ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tulizo Shemu akielezea maendeleo ya SACCOS hiyo wakati wa makabidhiano ya ofisi kwa Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge leo katika Taasisi hiyo iliyopo Jijini Dar es Salaam
Mwenyekiti wa chama cha wanawake wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Dkt. Angella Muhozya akimshukuru Prof. Mohamed Janabi kwa
kuwaongoza wanawake wa Taasisi hiyo wakati wa makabidhiano ya ofisi kwa
Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge leo katika Taasisi hiyo iliyopo
Jijini Dar es Salaam
Mkurugenzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) Prof.
Mohamed Janabi akiwashukuru wafanyaka wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa
ushirikano waliompa wakati wa uongozi wake wakati wa makabidhiano ya ofisi na Mkurugenzi
Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge leo katika Taasisi hiyo iliyopo Jijini Dar
es Salaam
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Willium Mahalu akiwapongeza wakugurenzi wapya wa JKCI na MNH wakati wa makabidhiano ya ofisi kwa Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge leo katika Taasisi hiyo iliyopo Jijini Dar es Salaam
Viongozi wa chama cha wanawake wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) wakimkabidhi zawadi ya picha aliyekuwa Mkurugenzi wa JKCI ambaye
sasa ni Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Prof. Mohamed
Janabi wakati akiwaaga wafanyakazi hao leo katika Taasisi hiyo iliyopo Jijini
Dar es Salaam
Baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) wakifuatilia yaliyokua yakiendelea wakati wa makabidhiano ya ofisi kwa
Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge leo katika Taasisi hiyo iliyopo
Jijini Dar es Salaam
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Prof. Willium Mahalu akiwa katika picha ya pamoja na wakurugenzi
wapya wa JKCI na MNH wakati wa makabidhiano ya ofisi kwa Mkurugenzi mpya wa
JKCI Dkt. Peter Kisenge leo katika Taasisi hiyo iliyopo Jijini Dar es Salaam
Picha na Khamis Mussa
***************************************************************************************
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imejipanga kuanzisha
mpango wa wananchi wote kufanya mazoezi ya kutembea na kukimbia ikiwa na kauli
mbiu ya “fanya mazoezi na JKCI kwa siku tatu za wiki linda moyo wako” ili
kupunguza magonjwa ya moyo ambayo yamekuwa yakiongezeka kwa kasi katika jamii.
Akizungumza wakati wa makabidhiano ya ofisi leo Jijini Dar es
Salaam Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter
Kisenge alisema kwa kushirikiana na wizara ya afya atahakikisha suala la
mazoezi linapewa kipaumbele ili kujenga jamii yenye afya bora.
Dkt.Kisenge alisema ataiomba Wizara ya afya kwa pamoja wawe na slogani ya kufanya mazoezi ya matembezi
nchi nzima ambapo wananchi ambao watatembea kilometa ambazo watakuwa
wamezipanga watapewa unafuu wa kufika JKCI kupatiwa matibabu ya moyo bila
malipo ikiwa ni njia ya kuwahamasisha wananchi kufanya mazoezi.
Akizungumzia uteuzi wa kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt.
Kisenge aliahidi kudumisha utendaji mzuri uliofanywa na Prof. Mohamed Janabi
tangu kuanzishwa kwa Taasisi hiyo miaka saba iliyopita kwa kuifanya Taasisi
hiyo kukuwa kwa kasi na kujulikana hapa Tanzania na nje ya nchi.
Dkt. Kisenge alisema JKCI itaendelea kuboresha huduma za
matibabu ya moyo hapa nchini kwa kuwawezeshea wananchi kupata huduma bora zaidi
na kuwafuata mahali walipo ili kuwapatia matibabu lakini pia kuwafundisha
madaktari waliopo mikoani ili waweze kujua jinsi gani wanaweza kuwasaidia
wagonjwa wa moyo.
“Tutaongeza vifaa tiba na miundombinu ambayo itawasaidia
madaktari wetu kuweza kufanya upasuaji wa moyo kwa njia za kisasa zaidi lakini
pia kupitia mtambo wetu wa Cathlab upande wa electrophysiology ambao
umenunuliwa na Serikali ya awamu ya sita nitaenda kuusimamia ipasavyo ili
wananchi waweze kupata huduma ya matibabu ya umeme wa moyo hapa nchini na
kupunguza gharama kubwa ambayo serikali ilikuwa inatumia kupeleka wagonjwa nje
ya nchi”,
Akizungumza wakati wa makabidhiano ya ofisi aliyekuwa
Mkurugenzi Mtendaji JKCI ambaye kwa sasa ni Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya
Taifa Muhimbili (MNH) Prof. Mohamed Janabi aliahidi kuendelea kushirikiana na
JKCI na kumuomba Mkurugenzi mpya kuiendeleza Taasisi hiyo pale alipoiacha.
Kwa upande wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Prof. Janabi alisema
kikubwa atakachokwenda kukifanya ni pamoja na kuboresha huduma zinazotolewa na
hospitali hiyo ili huduma ziweze kuendana na hadhi ya jina la hospitali ya
taifa.
“Huduma ambazo naenda kuziboresha kuanzia leo ni pamoja na
huduma ile ya mtu aliyefariki katika hospitali zetu zote zilizopo eneo la
muhimbili atakuwa anachukuliwa na gari la wagonjwa kupelekwa chumba cha
kuhifadhia maiti lakini pia wagonjwa wanaotoka kitengo cha dharura kupelekwa
mawodini kuanzia leo watakuwa wanabebwa na gari hilo badala ya kupelekwa kwenye
vitanda”,.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya JKCI Prof. William
Mahalu alisema anaamini Mkurugenzi aliyeteuliwa kuiongoza JKCI atafanya vizuri
kwani amekuwa akifanya naye kazi kwa muda mrefu hivyo kumtaka kuendeleza yale
yaliyoachwa na mkurugenzi aliyemaliza muda wake.
“Nawaomba wafanyakazi wamuunge mkono na kushirikiana na
Mkurugenzi mteule kwa kila hali kama ambavyo walikuwa wakishirikiana na
mkurugenzi aliyemaliza muda wake, ninachofurahi ni kwamba watumishi wa hapa
wanamfahamu mkurugenzi mteule hivyo haitakuwa ngumu kufanya naye kazi”,.
“Ahadi zilizotolewa na Mkurugenzi mpya naamini zote zina nia
ya kuboresha huduma na kung’arisha nyota ya taasisi hii, mimi kama mwenyekiti
wa bodi nimezichukuwa na nitazisimamia kuhakikisha kuwa ahadi hizo zinatekelezwa”,
alisema Prof. Mahalu
Comments
Post a Comment