Kigoma wapata elimu ya magonjwa ya moyo
Afisa Masoko wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Ireen Mbonde akimweleza Katibu Tawala wa mkoa wa Kigoma Hassan Rugwa huduma zinazotolewa na Taasisi hiyo wakati wa uzinduzi wa mradi wa lishe mtambuka unaofadhiliwa na Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID). Kulia ni Mratibu wa Huduma za Kitabibu wa Mratibu wa Huduma za Afya Mkoa wa Kigoma Dkt.Frank Sudai. Wataalamu wa JKC wako mkoani Kigoma kwaajili ya kufanya kambi maalumu ya upimaji na matibabu ya moyo inayofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Maweni – Kigoma.
*******************************************************************************************************************************************************************************************************************
Wakazi wa mkoa wa Kigoma wameishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kutoa elimu ya jinsi ya kuepukana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo.
Shukrani hizo wamezitoa leo mkoani humo wakati wa uzinduzi wa mradi wa
lishe mtambuka unaofadhiliwa na Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa
(USAID) ambapo JKCI ilishiriki katika maonesho na kutoa uelewa kwa wananchi kuhusu magonjwa ya
moyo pamoja na huduma wanazozitoa.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na mwandishi wa habari hizi
wananchi waliotembelea banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) walisema elimu waliyoipata itawasaidia kuweza
kuepukana na magonjwa ya moyo na wataitumia kuwaelimisha wengine.
“Binafsi sikuwa najua kuwa watoto wanaweza kuzaliwa na
magonjwa ya moyo lakini baada ya kufika hapa nimefahamu kuwa kuna watoto wanazaliwa
na magonjwa hayo na nimeelezwa namna ambavyo mama anaweza kufanya ili asiwe
katika hatari ya kuzaa mtoto mwenye magonjwa
ya moyo”, alisema John Kwigeza mkazi wa Maweni.
“Mimi na wanafunzi wenzangu tumetembelea banda la Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) tumejifunza jinsi mtu anavyoweza kupata magonjwa ya
moyo kama vile kutanuka kwa moyo na kuziba kwa mishipa ya damu ya moyo lakini
pia tumefundishwa namna ya kuepukana na magonjwa haya”.
“Elimu niliyoipata itanisaidia kuwafundisha wenzangu kuhusu
magonjwa ya moyo pia imenipa hamasa ya kusoma kwa bidii ili hapo baadaye niwe daktari
bingwa wa moyo”, alisema Sauda Adamu mwanafunzi wa kidato cha pili shule ya
sekondari Kigoma Ujiji.
Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wako mkoani humo kwaajili ya kufanya kambi maalumu ya siku tatu ya upimaji na matibabu ya moyo inayofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Maweni – Kigoma.
Comments
Post a Comment