Arusha wajitokeza kupima moyo
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dickson Minja akimwelezea huduma zinazotolewa katika banda la Taasisi hiyo mwananchi aliyetembelea banda la JKCI wakati wa maonesho ya kimataifa ya usalama mahala pa kazi yanayofanyika katika viwanja vya General tire vilivyopo jijini Arusha.
*********************************************************************************************************
Wananchi wa Mkoa wa Arusha wajitokeza kufanya uchunguzi wa
magonjwa ya moyo, shinikizo la damu, sukari kwenye damu na uwiano wa urefu na
uzito katika banda la Tasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
Uchunguzi huo unafanyika katika banda la Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) lililopo katika maonesho ya kimataifa ya usalama na afya
mahali pa kazi katika viwanja vya General tire vilivyopo jijini Arusha.
Akizungumza alipotembelea banda la JKCI mkazi wa Arusha Aika
Msuya alisema amevutiwa kupima moyo wake kwani amekuwa akipata maumivu makali
ya kifua tatizo ambalo hajawahi kufuatilia kama ni shida ya moyo au ni tatizo
lingine.
“Nashukuru baada ya kufanyiwa vipimo nimekutwa salama na kupewa
ushauri wa kuwa nafanya uchunguzi wa afya mara kwa mara, kufanya mazoezi na
kula mlo kamili”, alisema Aika
Aika alisema matembezi yake katika maonesho hayo yamekuwa
yamafanikio kwani hakutegemea kama angepata nafasi ya kupima moyo kama
isingekuwa kupitia maonesho hayo.
Grace Kitundu mkazi wa Arusha alisema yeye kama mama lishe
analo jukumu la kuiokoa jamii isipate magonjwa ya moyo kwa kujitahidi kutumia
mafuta kidogo ambayo ni safi na salama kwa afya.
“Nimefurahi leo nimefika katika banda la JKCI na kupata elimu
nzuri ambayo inaenda kunibadilisha katika kazi zangu kwani sisi kama mama lishe
tumekuwa tukiandaa vyakula vya wateja wetu bila ya kuangalia usalama wa afya”,
alisema Grace
Grace alisema anaenda kuwa mwalimu kwa wenzake wanaofanya
biashara ya chakula hasa eneo la matumizi ya chumvi nyingi wakati wa kuandaa
chakula ili kuwalinda wateja wanaowahudumia.
Naye Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dickson Minja alisema Taasisi hiyo itakuwepo katika
maonesho hayo hadi tarehe 30 Aprili 2024 ikitoa huduma za uchunguzi wa magonjwa
ya moyo, shinikizo la damu na sukari kwenye damu kwa watu wote watakaotembelea
banda la JKCI bila gharama.
Dkt. Dickson alitoa wito kwa vijana ambao umri wao umeanza
kusogea na watu ambao bado hawajapata changamoto za moyo kuchunguza afya zao,
kubadili mifumo ya maisha kujikinga kupata changamoto za magonjwa
yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo.
Comments
Post a Comment