Zaidi ya watu 11,250 wafikiwa na huduma ya tiba mkoba ya matibabu ya kibingwa ya moyo

Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Eva Wakuganda akizungumza na waandishi wa habari leo mkoani Kigoma kuhusu kambi maalumu ya siku tatu ya upimaji na matibabu ya moyo inayofanywa na  wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Maweni.

Mratibu wa Huduma za Afya Mkoa wa Kigoma Dkt.Frank Sudai akizungumza na waandishi wa habari leo mkoani humo kuhusu kambi maalumu ya siku tatu ya upimaji na matibabu ya moyo inayofanywa na  wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa – Maweni.

 Wananchi wa mkoa wa Kigoma wakisubiria kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo zinazotolewa na wataalamu wa  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa – Maweni katika kambi maalumu ya siku tatu ya uchunguzi na matibabu ya moyo inayofanyika katika hospitali hiyo.

 Mratibu wa Huduma za Kitabibu wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa – Maweni Dkt.Boniphace Kilangi akizungumza na waandishi wa habari leo mkoani Kigoma kuhusu kambi maalumu ya siku tatu ya upimaji na matibabu ya moyo inayofanywa na  wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa hospitali hiyo.

Wataalamu wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa – Maweni wakiwahudumia wananchi waliofika katika hospitali hiyo kwaajili ya kupata huduma za upimaji na matibabu ya moyo zinazotolewa na  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wataalamu hao katika kambi maalumu ya matibabu ya siku tatu.

*******************************************************************************************************************************************************************************************

Zaidi ya Wananchi 11,250 wamefikiwa na huduma ya tiba mkoba ya matibabu ya kibingwa ya moyo kwa kufuatwa mahali walipo ijulikanayo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services inayotolewa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Hayo yamesemwa leo na daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Eva Wakuganda wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kambi maalumu ya upimaji na matibabu ya moyo inayotolewa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa – Maweni.

Dkt. Eva alisema kutolewa kwa huduma hiyo katika mikoa 13 ya Tanzania Bara na Visiwani kumewasaidia wananchi wengi kupata huduma za matibabu ya kibingwa ya moyo kwa wakati tofauti na ambavyo wangezifuata huduma hizo jijini Dar es Salaam.

“Kwa wiki hii kuna watalaamu wa JKCI ambao tuko hapa Kigoma, wenzetu wako Iringa na wengine wako Chato huko kote tunatoa huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya moyo pamoja na elimu ya jinsi ya kuepukana na magonjwa haya”.

“Magonjwa yasiyo ya kuambukiza yakiwemo ya moyo yanaweza kuepukika kwa kufuata ushauri wa kitaalamu ikiwa ni pamoja na kufanya mazoezi, kutokutumia bidhaa aina ya tumbaku, kula chakula bora na kutokunywa pombe kupitiliza”, alisema Dkt. Eva.

Dkt. Eva alisema huduma hiyo ni endelevu kutokana na Taasisi hiyo kufika katika mikoa 13 na baadhi ya wilaya na kuwa na malengo ya kufika katika mikoa yote ambayo bado haijafika.

“Tunaishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuboresha huduma za afya kwa kununua vifaa tiba vya kisasa pamoja na kuendelea kuwasomesha wataalamu katika kada ya afya, kutokana na uwekezaji huo matibabu ya kibingwa yanafanyika hapa nchini tofauti na zamani ambapo wagonjwa walikuwa wanatibiwa nje ya nchi”, alishukuru Dkt. Eva.

Kwa upande wake Mratibu wa Huduma za Afya Mkoa wa Kigoma Dkt.Frank Sudai aliishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kuwatuma wataalamu wake  katika mkoa huo ambao wanashirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa - Maweni kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo kwa wananchi.

“Ninawaomba wananchi wa mkoa wa Kigoma na maeneo ya jirani kutumia fursa hii kufika hospitalini hapa kupata huduma ya uchunguzi na matibabu ya moyo kwani huduma hii imesogezwa karibu na kuwapunguzia gharama kama wangesafiri na kuifuata jijini Dar es Salaam”, alisema Dkt.Sudai.

Akizungumza kwa niaba ya Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa – Maweni Dkt. Stanley Binagi, Mratibu wa Huduma za Kitabibu wa Hospitali hiyo Dkt.Boniphace Kilangi alisema kufanyika kwa kambi hiyo pia kunawajengea uwezo wataalamu wa hospitali hiyo wa kuwatambua na kuwatibu wagonjwa wa moyo.

“Kambi hii ni nzuri kwani kila mtaalamu wa JKCI anafanya kazi na mtaalamu wetu wa hapa hii ikiwa ni pamoja na kufanya vipimo vya moyo na kuwatibu wagonjwa ninaamini ujuzi wanaoupata wataalamu wetu utatusaidia katika kutoa huduma za matibabu ya moyo kwa wagonjwa pindi wenzetu wa JKCI watakapoondoka”, alisema  Dkt. Kilangi.

Katika kambi hiyo ya siku tatu wananchi wanapata huduma mbalimbali za uchunguzi na matibabu ya moyo ikiwa ni pamoja na kupewa elimu ya lishe bora na matumizi sahihi ya dawa za moyo, kupimwa uwiano baina ya urefu na uzito, shinikizo la damu, kiwango cha sukari kwenye damu, kupimwa vipimo vya kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi pamoja na mfumo wa umeme wa moyo.


 


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari