JKCI na SACH kuokoa maisha ya watoto 20 Zambia kwa kufanya upasuaji wa moyo




Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Mkurugenzi wa Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (SACH) la nchini Israel Simon Fisher wakiwa katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Kambarage Nyerere jana kuanza safari ya kwenda nchini Zambia kwaajili ya kambi maalumu ya siku sita ya upasuaji wa moyo kwa watoto inayoanza leo katika Hospitali ya Taifa ya Moyo Zambia (NHH).


Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Mkurugenzi wa Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (SACH) la nchini Israel Simon Fisher wakiwa katika picha ya pamoja walipowasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kenneth Kaunda uliopo nchini Zambia jana kwaajili ya kufanya kambi maalumu ya siku sita ya upasuaji wa moyo kwa watoto inayoanza leo katika Hospitali ya Taifa ya Moyo Zambia (NHH).


Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao wa Hospitali ya Taifa ya Moyo Zambia (NHH) wakiwa katika kikao cha kujadili watoto watakaofanyiwa upasuaji wa moyo katika kambi maalumu ya siku sita ya upasuaji wa moyo kwa watoto inayoanza leo katika Hospitali ya Taifa ya Moyo Zambia (NHH).

Na JKCI

***********************************************************************************************

Madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao kutoka Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto la nchini Israel (SACH) kufanya kambi maalumu ya upasuaji wa moyo kwa watoto 20 wa nchini Zambia.

Kambi hiyo ya siku sita inaanza leo katika Hospitali ya Taifa ya Moyo ya nchini Zambia (NHH) kwa kushirikiana na wataalamu wa Hospitali hiyo, na daktari wa usingizi kutoka nchini Ethiopia.

Akizungumza na mwandishi wa habari hii jana nchini Zambia Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Godwin Sharau alisema katika kambi hiyo utafanyika upasuaji wa kufungua kifua pamoja na upasuaji wa  tundu dogo kwa kutumia mtambo wa Cathlab.

“Kambi hii inafanyika kwa kushirikiana na wataalamu kutoka nchini Tanzania, Zambia, Ethiopia, na Israel wote tukiwa na lengo la kuwasaidia watoto wenye magonjwa ya moyo waliopo nchini Zambia”, alisema Dkt. Godwin

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (SACH) la nchini Israel Simon Fisher alisema Shirika hilo limeandaa kambi hiyo kuwasaidia wataalamu wa afya wa nchini Zambia na kuwajengea uwezo katika kutoa huduma za matibabu ya moyo kwa watoto.

Simon alisema JKCI, na SACH wamekuwa na ushirikiano wa muda mrefu tangu kuanzishwa kwa Taasisi hiyo mwaka 2015 hivyo kupitia ushirikiano huo wamepanga kwa pamoja kuwasaidia watoto wenye magonjwa ya moyo waliopo nchini Zambia.

“SACH imeweza kuwajengea uwezo madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa JKCI kwa kipindi cha muda mrefu, na baadaye kuanza kuwajengea uwezo wataalamu wa Hospitali ya Moyo Zambia hii yote ni kuhakikisha huduma bingwa bobezi za magonjwa ya moyo kwa watoto zinapatikana katika nchi hizi”, alisema Simon


Comments

Popular posts from this blog

Wateja wa CRDB kutibiwa JKCI kwa punguzo la asilimia 50%

Wanawake wa JKCI SACCOS wanaongoza kwa kumiliki hisa

JKCI, MOI NA MNH waitwa Comoro kutoa huduma za matibabu ya kibingwa