JKCI yazindua mfumo wa kidigitali wa miadi ya wagonjwa


Afisa Tehama wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Alamin Msangi akimuelekeza mgonjwa namna ya kuchukua token katika kioski baada ya mgonjwa kufunya miadi ya kumuona daktari kupitia simu janja. 

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Tehama wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Fiona Kavishe akionesha tovuti yenye mfumo wa kidigitali wa miadi mtandao.


Afisa Tehama wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Alamin Msangi akifuatilia namna ambavyo ndugu wa mgonjwa aliyelazwa JKCI anavyochukua token katika kioski kabla ya ndugu huyo kuingia kumuona mgonjwa.

Na JKCI

*********************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imeanzisha mifumo miwili ya kisasa ya kuweka miadi kwa ajili ya kumuona daktari na mfumo wa namna ndugu wa mgonjwa anavyoweza kumtembelea mgonjwa aliyelazwa hospitalini.

Mifumo hiyo inapatikana kupitia tovuti rasmi ya taasisi hiyo (www.jkci.or.tz) ambapo wagonjwa sasa wanaweza kuweka miadi ya kumuona daktari kwa urahisi kwa kubofya sehemu ya Appointments na kuchagua tarehe, muda pamoja na aina ya huduma wanayohitaji.

Akizungumzia mfumo huo Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Tehama wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Fiona Kavishe alisema uanzishwaji wa mfumo huo umelenga kupunguza msongamano wa wagonjwa na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma zinazotolewa na Taasisi hiyo.

 “Faida ya mfumo wa miadi ya kumuona daktari utamsaidia wananchi kumuona daktari yoyote anayemtaka tofauti na awali ilikuwa wagonjwa baadhi wanamuona daktari huyo huyo”, alisema Fiona

Fiona alisema kupitia mfumo wa kutembelea wagonjwa waliolazwa wodini, ndugu wa wagonjwa wanaotaka kuwatembelea wagonjwa waliolazwa hospitalini wanaweza kutumia mfumo huo kwa kubofya sehemu ya Visitor kuchagua tarehe ya kuwatembelea wagonjwa na kufuata taratibu zilizowekwa.

 Kwa upande wake Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Salehe Mwinchete alisema mfumo huo utawarahisishia madaktari kupanga ratiba zao vizuri na kuweza kufahamu kwa siku wana idadi ya wagonjwa wangapi tofauti na awali ilikuwa ngumu kwao kuweka ratiba zao vizuri.

Dkt. Salehe alisema wagonjwa wakitumia mfumo wa miadi ya kumuona daktari kutasaidia kupunguza malalamiko ya wao kukaa muda mrefu hospitali kusubiri huduma lakini pia kutawapa muda wa kupumzika na kuacha tabia ya kuamka mapema kuwahi foleni ya kumuona daktari.

Naye mgonjwa aliyefanikiwa kufanya miadi kupitia tovuti hiyo Wenceslous Shoo alisema mfumo huo ni mzuri na una faida nyingi kwa wagonjwa kwani watakuwa na muda mchache wa kukaa hospitali.

“Huduma hii ya kuweka miadi mtandaoni ni mzuri kwasababu inapunguza usumbufu wa kupanga foleni na kuamka alfajiri sana, ningeomba elimu itolewe na kuwafikia watu wengi zaidi ili waweze kuutumia mfumo huu” alisema Shoo. 

Mfumo wa kidigitali wa kuweka miadi ya kumuona daktari na kutembelea wagonjwa waliolazwa JKCI umeanzishwa ili kuimarisha huduma kwa wananchi, kuongeza uwazi na kuhakikisha usalama wa wagonjwa walipoko wodini kwa kudhibiti idadi ya wageni.


Comments

Popular posts from this blog

Wateja wa CRDB kutibiwa JKCI kwa punguzo la asilimia 50%

Wanawake wa JKCI SACCOS wanaongoza kwa kumiliki hisa

JKCI, MOI NA MNH waitwa Comoro kutoa huduma za matibabu ya kibingwa