Watu 420 wapimwa moyo Manyara
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Johnstone Kayandabila akimpima kipimo cha kuangalia jinsi moyo
unavyofanyakazi (Echocardiogram – ECHO) mwananchi wa Manyara aliyefika katika
Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Manyara (MRRH) kwa ajili ya kupima moyo wakati wa
kambi maalum ya siku tano ya matibabu ya moyo iliyokuwa ikifanywa na wataalam
wa afya wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa MRRH na kumalizika leo Mkoani
Manyara
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mohamed
Wamara akimpima kipimo cha kuangalia jinsi mfumo wa umeme wa moyo unavyofanya
kazi (Electrocardiography – ECG) Glory Ifunya aliyefika katika Hospitali ya
Rufaa Mkoa wa Manyara (MRRH) kwa ajili ya kupima moyo wakati wa kambi maalum ya
siku tano ya matibabu ya moyo iliyokuwa ikifanywa na wataalam wa afya wa JKCI
kwa kushirikiana na wenzao wa MRRH na kumalizika leo Mkoani Manyara
Jumla ya watu 420 wamefanyiwa uchunguzi na matibabu ya
magonjwa ya moyo katika kambi maalum ya siku tano iliyoanza tarehe 15 Mei 2023
na kumalizika leo katika Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Manyara (MRRH).
Kambi hiyo iliyofanywa na wataalam wa afya wa Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa Mkoa wa
Manyara (MRRH) imewahudumia watu wazima 390 na watoto 30.
Akizungumza wakati wa kufunga kambi hiyo Daktari bingwa wa
magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Johnstone Kayandabila
alisema katika kambi hiyo wametoa rufaa kwa wagonjwa wa moyo 99 ambapo kati yao
wagonjwa 10 walikuwa watoto na wagonjwa 89 walikuwa watu wazima ili waweze
kufika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa ajili ya matibabu zaidi.
“Sababu za kutoa rufaa kwa wagonjwa hao ilikuwa ni pamoja na
matatizo mbalimbali yanayotokana na athari za magonjwa ya shinikizo la juu la
damu, sukari kuwa juu, mishipa ya damu kuziba pamoja na valvu za moyo
kutokufanya kazi vizuri”,
“Magonjwa mengine tuliyokutana nayo wakati wa kambi hii ni
matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo kutokufanya kazi vizuri na magonjwa ya moyo
ya kuzaliwa nayo kwa watoto yaani matundu kwenye moyo”, alisema Dkt. Johnstone
Aidha Dkt. Johnstone alitoa wito kwa wagonjwa waliopewa rufaa
kufika JKCI ili waweze kupatiwa matibabu kwa haraka kupunguza athari
zitakazoweza kujitokeza kama hawatapata matibabu kwa wakati.
Naye Mganga Mfadhiwi Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Manyara Dkt.
Catherine Magali amewapongeza madaktari bingwa wa moyo kutoka JKCI kwa kutoa
huduma kwa wananchi wa Manyara kwani huduma hizo ni muhimu kufanyika mara kwa
mara.
“Kuwapata watu 99 rufaa
kwa wiki moja sio kazi ndogo, mmefanya kazi ya ziada kwani watu hawa
wangeendelea kuishi tu huku bila ya kujua yakuwa walihitaji matibabu ya haraka
kuokoa maisha yao”, alisema Dkt. Catherine
Dkt. Catherine ambaye pia ni bingwa wa magonjwa ya wanawake
MRRH alisema mwanzo wa ushirikiano uliojengwa katika kambi hiyo uendelee hata
pale Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Manyara itakapowahitaji tena mabingwa hao
kutoka JKCI wasisite kushirikiana nao.
Comments
Post a Comment