JKCI kufanya maadhimisho ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwake

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 10 ya JKCI uliofanyika hivi karibuni katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam

Baadhi ya viongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakisikiliza wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 10 ya JKCI uliofanyika hivi karibuni katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akipokea tuzo iliyotolewa na Shirika la Human of Global lililopo London nchini Uingereza kutambua mchango wake katika kuleta mabadiliko katika huduma za afya nchini wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 10 ya JKCI uliofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam.

**********************************************************************************************************

Taasisi ya moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kuadhimisha miaka 10 tangu kuanzishwa kwake kwa kufanya kampeni maalumu ya uhamasishaji wa magonjwa ya moyo nchini.

Maadhimisho hayo yanaanza rasmi tarehe 1 mwezi Agosti na kuhitimishwa tarehe 20 Septemba mwaka huu yatahusisha mhadhara wa umma kujadiliana kuhusu tiba utalii nchini pamoja na kufanya bonanza la wafanyakazi wa Taasisi hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari hivi karibuni jijini Dar es saalamu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema Taasisi hiyo inaadhimisha miaka 10 kutokana na mafanikio iliyoyapata katika kutoa huduma bingwa bobezi za uchunguzi na matibabu ya moyo nchini.

Dkt. Kisenge alisema kwa kipindi cha miaka 10 JKCI imeweza kutoa huduma za upasuaji wa moyo wa kisasa kupitia mtambo wa Cathlab (Catheterization Laboratory) na kuweza kubadilisha valvu ya mshipa mkubwa wa damu (Aortic Valve) bila kufungua kifua.

Mafanikio mengine ambayo taasisi hiyo imeyapata ni pamoja na kuongeza utaalamu katika kutoa huduma za upasuaji wa moyo, kuanzisha program za uhamasishaji na uchunguzi kupitia huduma ya tiba mkoba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kushirikiana na mataifa mbalimbali duniani, kufanya tafiti na mafunzo kwa wataalamu wa afya pamoja na kuwekeza katika vifaa tiba vya kisasa.

Aidha Dkt. Kisenge alisema JKCI katika kuendelea kuboresha huduma za matibabu ya moyo imeweka mikakati ya baadaye ikiwemo kuwa na jengo la watoto wenye matatizo ya moyo eneo la Mloganzila, kuimarisha huduma kwa kuongeza huduma za matibabu ya moyo katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato, Lumumba Zanzibar, na Arusha Lutheran (Seriani), kuendeleza utafiti pamoja na kupandikiza moyo.

Kwa upande wake mwenyekiti wa maadhimisho ya miaka 10 ya JKCI Dkt. Naizihijwa Majani alisema kampeni zinazofanywa na Taasisi hiyo wakati wa kuadhimisha miaka 10 ya JKCI zitaenda sambamba na kampeni ya kuzuia magonjwa ya moyo kwa watoto kwa kutoa elimu ya afya na uchunguzi wa moyo kwa wanafunzi katika shule za sekondari.

Dkt. Naizihijwa alisema katika mhadhara utakaofanyika wakati wa maadhimisho hayo JKCI imepanga kujadili umuhimu wa tiba utalii nchini na manufaa yake kwa wananchi, nafasi ya mashirika ya umma katika tiba utalii pamoja na mafanikio ya tiba utalii baada ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo.

“Mhadhara utakaofanywa na Taasisi yetu kuhusu tiba utalii nchini utaongozwa na wataalamu bobebi kutoka sekta ya afya pamoja na sekta ya utalii nchini”, alisema Dkt. Naizihijwa

Maadhimisho ya miaka 10 ya JKCI yenye kauli mbiu “Tumethubutu, Tumeweza Tunasonga mbele” yanatarajiwa kuambatana na matukio mbalimbali ya kitaaluma, utafiti, huduma za kijamii, pamoja na uzinduzi wa mikakati mipya ya kuboresha huduma za moyo nchini.


Comments

Popular posts from this blog

Wateja wa CRDB kutibiwa JKCI kwa punguzo la asilimia 50%

Wanawake wa JKCI SACCOS wanaongoza kwa kumiliki hisa

JKCI, MOI NA MNH waitwa Comoro kutoa huduma za matibabu ya kibingwa