Kambi ya matibabu ya moyo yaacha tabasamu kwa wananchi wa Shinyanga

 Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimkabidhi dawa mkazi wa Shinyanga aliyefika katika Hospitali ya Rufaa Mkoa Shinyanga (SRRH) kwaajili ya kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo  zilizokuwa zinatolewa hivi karibuni na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa SRRH.

Fundi sanifu wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Paskal Kondi akimfanyia mwananchi kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi wakati wa kambi maalumu ya matibabu ya moyo ya siku tano iliyofanywa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa Mkoa Shinyanga (SRRH).


Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mohamed Aloyce akizungumza na mwananchi wa Shinyanga kuhusu matumizi sahihi ya dawa wakati wa kambi maalumu ya Tiba Mkoba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services inayofanywa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kiketwe (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Shinyanga (SRRH).


Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Nuru Letara akimwelekeza Ayubu Burugu mkazi wa Shinyanga tatizo la moyo alilokuwa nalo mtoto wake aliyefika kupimwa na kupatiwa matibabu ya moyo katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga (SRRH) wakati wa kambi maalum ya siku tano ya Tiba Mkoba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyomalizika hivi karibuni.

Baadhi ya wakazi wa Shinyanga wakisubiri kupata huduma za upimaji na matibabu ya moyo zilizokuwa zinatolewa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa Mkoa Shinyanga (SRRH) wakati wa kambi maalumu ya siku tano ya Tiba Mkoba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyomalizika hivi karibuni.

**********************************************************************************************************************************************************************

Watu 502 wamepata huduma ya uchunguzi na matibabu ya moyo katika  kambi maalum ya matibabu  iliyofanyika kwa siku tano katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa  Shinyanga (SRRH).

Kambi hiyo ilifanywa na wataalamu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Shinyanga (SRRH).

Akizungumza na waandishi wa habari hivi karibuni Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa Mkoa Shinyanga (SRRH) Dkt. Luzila John alisema kati ya watu waliowaona watu wazima walikuwa 437 na watoto 65.

“Watu wote hawa walifanyiwa vipimo vya maabara vya kuangalia matatizo mbalimbali yanayoweza kusababisha magonjwa ya moyo. Watu 328 tuliwafanyia  kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi na watu 287 waliwafanyia  kipimo cha kuangalia mfumo wa umeme wa moyo”.

“Kati ya wagonjwa tuliowaona kuna ambao walikutwa na matatizo makubwa ya moyo ambayo yalihitaji matibabu ya kibingwa hivyo tumewapa rufaa ya kwenda kutibiwa JKCI, idadi yao ni  100 watu wazima wakiwa 63 na watoto 37”, alisema Dkt. John.

Dkt. John alisema lengo la kambi hiyo ilikuwa ni kusogeza huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo karibu zaidi na wananchi wa mkoa wa Shinyanga ili kuwapunguzia gharama za usafiri za kwenda Dar es Salaam.

“Wataalamu wetu wa  afya wapatao 16 wamepata mafunzo ya namna ya kufanya uchunguzi wa moyo na kutoa huduma za awali, hii ni fursa muhimu kwa hospitali ya mkoa na halmashauri za mkoa wa Shinyanga”, alisema Dkt. John.

Kwa upande wake daktari bingwa wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group, Mlagwa Yango alisema wagonjwa wengi waliwakuta na tatizo la Shinikizo la juu la damu, moyo kutanuna, moyo kushindwa kufanya kazi vizuri, matatizo ya valvu, mishipa ya damu  ya moyo na matundu kwa watoto.

Dkt. Yango alisema kufanyika kwa kambi hiyo kumewasaidia  wananchi kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo kwa haraka zaidi tofauti na ambavyo wangezifuata Dar es Salaam kwani kuna gharama za usafiri.

 “Tunapowahudumia wananchi kwa kuwafuata mikoani mikoani tunawarahisishia kupata huduma na kupunguza idadi ya wagonjwa wanaolazimika kusafiri umbali mrefu kufuata matibabu”,  alisema  Dkt. Yango.

Nao wananchi waliopata huduma ya uchunguzi na matibabu ya moyo katika kambi hiyo walishukuru kwa huduma waliyoipata na  kuomba huduma hiyo ifanyike mara kwa mara.

 “Huduma ni nzuri  ila tunaomba ziwe endelevu, mara nyingi ni gharama kubwa kwenda Dar es Salaam kupata huduma hizi hivyo ujio wa madaktari bingwa unatupunguzia mzigo mkubwa wa kufuata matibabu Dar es Salaam”,  alisema Damas Kimaro mkazi wa Manispaa ya Shinyanga.

 “Huduma tumepokea vizuri madaktari na wauguzi wametuhudumia bila rushwa wala usumbufu nimefurahi na ninashukuru kwa kutuletea huduma hizi, zimekuwa msaada mkubwa kwani wengi hatuna uwezo wa kusafiri hadi Dar es Salaam”, alishukuru Happiness Bwire mkazi wa Majengo Mapya.

Kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya moyo mkoani Shinyanga ni sehemu ya programu ya Tiba Mkoba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services yenye lengo la kuwasogezea karibu wananchi huduma za kibingwa za matibabu ya moyo.

Comments

Popular posts from this blog

Wateja wa CRDB kutibiwa JKCI kwa punguzo la asilimia 50%

Wanawake wa JKCI SACCOS wanaongoza kwa kumiliki hisa

JKCI, MOI NA MNH waitwa Comoro kutoa huduma za matibabu ya kibingwa